September 19, 2024

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Mil. 300 zakusanywa mbio za NBC Dodoma Marathon

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa jana Jumapili ameongoza washiriki zaidi ya 12,000 wa mbio za NBC Dodoma Marathon zilizofanyika kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma huku akiwapongeza waandaaji wa mbio hizo Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) kwa kufanikiwa kukusanya fedha kiasi cha Sh 300 milioni zitakazoelekezwa katika kuokoa maisha ya mama na mtoto. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).

Katika mbio hizo zilizohusisha washiriki kutoka ndani na nje ya nchi, ilishuhudiwa washiriki kutoka Tanzania, Kenya na Uganda wakichuana vikali kwa kuibuka washindi kwenye mbio tofauti hususani zile za km 10, km 21 na km 42. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa aliwaongoza viongozi mbalimbali wakiwemo wa kitaifa na viongozi wa taasisi na mashirika mbalimbali walioshiriki kwenye mbio za KM 5.

Akizungumza kwenye hafla ya kukabidhi zawadi kwa washindi na wadau mbalimbali wa mbio hizo, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa pamoja na kuipongeza benki ya NBC kwa mafanikio hayo, alionyesha kuguswa na ongezeko kubwa la washiriki wa mbio hizo kutoka washiriki 1,500 mwaka 2020 hadi kufikia washiriki 8,000 waliojiandikisha rasmi kushiriki mbio hizo mwaka huu.
Hatua hiyo alisema inasadifu mwamko mkubwa wa wananchi kushiriki katika michezo hatua ambayo itasaidia katika kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo ugonjwa wa moyo, kisukari na figo.

“Mchango wa Benki ya NBC katika kuinua sekta ya michezo nchini upo wazi sana ambapo wametenga fedha zaidi ya bilioni 36 katika kufanikisha udhamini wa michezo mbalimbali ikiwemo mchezo wa mpira wa miguu,” alisema.

Awali akizungumza kwenye hafla hiyo, Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamis Mwinjuma pamoja na kuipongeza benki hiyo kwa kuwa mdau mkubwa wa sekta ya michezo hapa nchini kupitia jitihada zake mbalimbali, alisema ukubwa wa mashindano hayo ya NBC Dodoma Marathon unatoa fursa kwa mamlaka zinazosimamia mchezo huo kutumia washindi mbalimbali waliopatikana kwenye mbio hizo kuliwakilisha taifa kwenye mashindani mbalimbali ya kimataifa yakiwemo mashindano ya Olympics na yale ya Jumuiya ya Madola (Commonwealth).

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC, Theobald Sabi alisema kiasi cha Sh 300 milioni kilichokusanywa kupitia mbio kitaelekezwa katika kufanikisha malengo ya mbio hizo ambayo ni ukusanya fedha ili kusaidia mapambano dhidi ya saratani ya shingo ya kizazi kwa kushirikiana na Taasisi ya Saratani ya Ocean Road pamoja na kutoa ufadhili wa elimu kwa wakunga kupitia Taasisi ya Benjamin Mkapa lengo kuu likiwa ni kuboresha afya ya mama wa mtoto.

“Zaidi pia sehemu ya fedha hii itaelekezwa katika kufanikisha ujenzi wa chumba cha upasuaji wagonjwa kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Mafanikio haya yanachochewa na dhamira yetu kama benki ya kuwa mstari wa mbele katika kusaidia jamii tunayoihudumia.

“Pia nawapongeza sana wadau mbalimbali waliojitokeza kufanikisha mbio hizo wakiwemo Kampuni ya Bima ya Sanlam ambao ni wadhamini wakuu wa mbio hizo sambamba na kampuni ya mawasiliano ya Vodacom waliodhamini mbio za km 21 pamoja na wadhamini wengine wote waliotuunga mkono,” alisema.

About The Author