May 25, 2025

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Waziri Mkenda azindua Mashindano ya NBC ya Uandishi wa Insha, Wazo Bora la Biashara kwa wanafunzi

 

WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda (Mb) leo amezindua Mashindano ya Uandishi wa Insha na Wazo Bora la Biashara kwa wanafunzi wa Sekondari nchini yaani “NBC Essay Challenge” na “NBC Business Idea Competition’ yanayoratibiwa na Benki ya NBC kwa ushirikiano na serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).

Mashindano hayo ambayo yanatarajiwa kuwafikia zaidi ya wanafunzi milioni moja wa shule za sekondari za umma na binafsi nchini, yanalenga kuchochea fikra za ubunifu, utafiti na uthubutu miongoni mwa vijana, kuimarisha elimu ya fedha na ujasiriamali wa vitendo sambamba na kuweka msingi wa usimamizi bora wa rasilimali – majumbani na mashuleni huku yakitoa fursa kwa mshindi wa jumla kujishindia fedha taslimu kiasi cha sh mil 10.

Hafla ya uzinduzi wa mashindani hayo imefanyika leo Makao Makuu ya Benki ya NBC jijini Dar es Salaam ikihudhuriwa na wawakilishi kutoka Ofisi ya Rais–TAMISEMI, Wizara ya Elimu, wazazi, walimu na wanafunzi kutoka shule mbalimbali za jijini Dar es Salaam. Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi aliwaongoza wafanyakazi wengine kwenye hafla hiyo.

Akizungumza kwenye hiyo Prof. Mkenda pamoja na kuipongeza benki ya NBC kwa jitihada hizo alisema mashindano hayo ni fursa kwa wanafunzi kote nchini katika kupima na kuthibitisha ubora wa mawazo na mitazamo yao kwenye masuala mbalimbali muhimu ikiwemo kiuchumi.

“Ni kutokana na umuhimu wa mashindani haya kwa watoto wetu ndio maana natoa wito kwa watendaji wa Wizara kuhakikisha taarifa kuhusu mashindano haya zinafika kwenye shule zote hapa nchini ili kutoa fursa kwa wanafunzi wengi zaidi kuweza kushiriki” aliagiza Prof Mkenda.

“Zaidi niwapongeze sana Benki ya NBC kwa kuwa imeendelea kuwa kinara kwenye jitihada za kueneza elimu ya fedha kuanzia kwenye ngazi ya chini kabisa kijamii kwa kupitia kwenye shule. Jitihada hizi ni muhimu sana katika kuandaa kizazi kinachotambua na kuheshimu misingi ya kiuchumi kupitia nidhamu ya fedha na matumizi sahihi ya taasisi za kifedha katika kujijenga kiuchumi.” Aliongeza.

Awali akizungumza kwenye hafla hiyo Bw Sabi alisema kupitia mashindano hayo yaliyoandaliwa kwa ubunifu wa hali ya juu, benki hiyo inalenga kuwajengea wanafunzi misingi ya nidhamu ya kifedha, umuhimu wa kujiwekea akiba na kuwajengea ufahamu utakao waongezea ushindani katika soko la biashara.

“Tafiti za FINSCOPE 2023 zinaonesha kuwa ni asilimia 35 tu ya vijana wa umri wa chini ya miaka 25 ndio wenye wana akaunti ya benki. Hili ni jambo linaloashiria pengo kubwa katika elimu ya fedha hususan tukitambua ukweli kuwa hili ndio kundi kubwa zaidi nchini…NBC tupo hapa kutatua changamoto hii’’ Alisema Sabi

Kwa mujibu wa Bw Sabi, ili kuongeza ari ya ushiriki, shindano hilo litatoa zawadi mbalimbali zikiwemo pesa taslimu hadi shilingi milioni 10 kwa mshindi wa jumla, Kompyuta, simu za mkononi, vitabu, mabegi na vifaa vya kujifunzia, Wanafunzi 200 bora watapata fursa ya kujiunga na programu ya ‘NBC Student Mentorship Club” – ambayo ni mpango maalum wa kulea vijana na kuwapatia mafunzo ya elimu ya fedha na ujasiriamali wakati wa likizo zao.

Aidha, Bw Sabi aliwashukuru wadau wa kampeni hiyo ikiwemo kampuni ya APE Booksellers, kwa kutoa vitabu 3,000 pamoja na pesa taslimu kama sehemu ya zawadi.

Akizungumzia vigezo muhimu vya ushiriki katika shindano hilo Bw Sabi alisema ni mwanafunzi kuwa na akaunti ya Benki ya NBC kwa kuwa zawadi zote za fedha kwa washindi zitawekwa moja kwa moja kwenye akaunti za benki hiyo mahususi kwa wanafunzi ambazo ni NBC Student Account – kwa wanafunzi wa sekondari na vyuo na Chanua Account – kwa wanafunzi walio chini ya miaka 18.

Wakitoa maoni yao kuhusu mashindano hayo Mwalimu Ivan Danda kutoka Shule ya Sekondari ya Makongo ya jijini Dar es Salaam na wanafunzi Prosper Clifford na Nora Mawalla pamoja na kuishukuru benki hiyo kwa shindani hilo walisema litakuwajengea wanafunzi misingi ya nidhamu ya kifedha, umuhimu wa kujiwekea akiba na kuwajengea ufahamu utakao waongezea ushindani katika soko la biashara na ajira.

About The Author

error: Content is protected !!