September 28, 2024

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Lissu kumburuza Makonda The Hugue

Tundu Lissu, Makamu Mwenyekiti Chadema Bara

 

TUNDU Lissu,Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Chadema na Maendeleo nchini Tanzania, amesema ameapa kumburuza kwenye Mahakama za Kimataifa, Paul Makonda, aliyekuwa mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam. Anaripoti Saed Kubenea, Dar es Salaam …(endeelea).

Lissu anamtuhumu Makonda kwa kupanga, kufadhili na kutekeleza njama za mauwaji dhidi yake na watu wengine kadhaa waliouawa au kushambuliwa wakati wa utawala wa John Magufuli.

“Tayari nimemuelekeza mwanasheria wangu, Bob Amsterdam kuanza taratibu za kumshitaki Makonda kwa ugaidi aliyonifanyia,” ameeeleza kiongozi huyo wa upinzani ambaye ni mkosoaji mkubwa wa serikali.

Kwa sasa, Makonda ni mkuu wa mkoa wa Arusha.

Kiongozi huyo wa serikali ya sasa ya Rais Samia aliwahi kuulizwa na gazeti la MwanaHALISI kuhusiana na madai hayo na kujibu kwa ufupi, “kamuulize Mama yako.”

Aliongeza: “Makonda ndiye aliyewasindikiza wale wauaji. Aliwaleta hadi Dodoma ambako nikishambuliwa.”

Aidha, Lissu amesema atawaburuza mahakamani kampuni ya Millicom ambayo ilikuwa kampuni mama ya simu za mkononi ya Tigo na serikali ya Tanzania kwa tuhuma za kuhusika na jaribio la kutoa uhai wake.

Lissu ametoa kauli hiyo hayo baada ya mahakama moja nchini Uingereza kuelezwa kuwa kampuni ya mawasiliano ya Tigo (ambayo ilikuwa ikimilikiwa kwa wakati huo na Millicom), ilitoa taarifa za mawasiliano na nyendo za mwanasiasa huyo kwa saa 24 siku chache kabla ya tukio la kushambuliwa kwake.

Mbunge huyo wa zamani wa Singida Mashariki alishambuliwa kwa risasi tarehe 7 Septemba 2017, nyumbani kwake, Area D, mjini Dodoma, muda mfupi baada ya kutoka bungeni alikochangia mjadala wa asubuhi.

Hata hivyo, Lissu amesema hajui tarehe rasmi ya kuanza kwa kesi hiyo kwani mawakili wake wanahitaji kukusanya ushahidi wa kutosha.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Jumatano jion, Lissu ameeleza kwanini hakuwahi kufungua kesi dhidi ya Millicom.

“Sikwenda mahakamani kwasababu sikuwa na ushahidi wa kutosha. Lakini sasa tunao ushahidi unaotosheleza kufungua kesi” amesema Lissu.

Ushahidi wa kuhusika kwa kampuni ya Millicom umekuja baada ya kesi iliyofunguliwa mwaka 2019 dhidi ya kampuni hiyo nchini Uingereza na aliyekuwa mtumishi wa kampuni hiyo.

Lissu amelilaumu jeshi la polisi kwa kutokufanya uchunguzi wa tukio aliloliita la kigaidi.

“Hadi leo sijaitwa na polisi kuulizwa niliona nini. Wakati mimi niliwaona vijana wawili. Mtumishi wangu wa ndani aliyepo Dodoma na mtumishi wa Tulia Ackson aliyempeleka kwenye gari” alisema.

Amedai kuwa anaamini polisi hawajawahi hata kufungua jalada.

Kupatikana kwa taarifa kuwa Serikali ilishinikiza kampuni ya Tigo kutoa mawasiliano ya Lissu ambayo yalirahisisha shambulio dhidi yake, kunazidi kuizamisha serikali ya Tanzania katika lindi la tuhuma za mauaji, utekaji na utesaji ya wapinzani wa serikali.

About The Author