March 18, 2025

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Kamati ya Bunge yaitaka TAMISEMI kuchunguza mkandarasi wa mradi Tactic Kahama

Mwenyekiti wa Kamati Bunge, Justin Nyamoga

 

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya TAMISEMI imeielekeza Ofisi ya Rais – TAMISEMI kupitia upya mkataba wa mkandarasi wa kigeni, Sichuan Road and Bridge Group Corporation, na kuchukua hatua za haraka kutokana na kushindwa kutekeleza kwa wakati mradi wa TACTIC awamu ya kwanza katika Wilaya ya Kahama, Mkoa wa Shinyanga. Anaripoti Apaikunda Mosha, Shinyanga … (endelea).

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Justin Nyamoga, ametoa maelekezo hayo wakati wa ziara ya kamati hiyo ya kukagua utekelezaji wa mradi huo wa ujenzi wa barabara za katikati ya mji na mifereji ya maji ya mvua wenye thamani ya Sh. 20.864 bilioni.

Kwa mujibu wa mkataba, mradi huu ulianza kutekelezwa Novemba 20, 2023, na ulipaswa kukamilika Februari 19, 2025. Hata hivyo, hadi sasa utekelezaji wake uko katika asilimia 48%, hali iliyosababisha kuongezewa muda wa ziada wa miezi mitatu hadi Mei 19, 2025.

Naibu Waziri wa TAMISEMI, Zainab Katimba

Nyamoga amesema “Kamati haitatoa maelekezo nini kifanyike, lakini ninyi nendeni mkasome mkataba wake, kaangalieni changamoto anazozisababisha, ikiwemo kuwafilisi Watanzania ambao yeye amechukua vitu kwao na hajawalipa.”

Naye, Naibu Waziri wa TAMISEMI, Zainab Katimba, akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Mohamed Mchengerwa, amesema serikali itasubiri kwa miezi mitatu kuona kama mkandarasi huyo atakamilisha kazi na iwapo atashindwa, serikali itavunja mkataba na mkandarasi huyo hatakuwa na sifa ya kupata kazi nchini.

Kwa upande wake, Mhandisi Rogatus Mativila, Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais – TAMISEMI anayeshughulikia Miundombinu, amesema moja ya changamoto zinazokwamisha miradi mingi ni kuhamisha pesa za miradi kwenda kwenye shughuli nyingine baada ya kuzipokea.

Mradi huu wa Kupendezesha Miji (TACTIC) unatekelezwa katika Halmashauri 45 nchini, ikiwemo Kahama, ambapo awamu ya kwanza inahusisha, Ujenzi wa barabara za katikati ya mji – Kilomita 12.03, Barabara za eneo la viwanda Zongomela – Kilomita 3.06, Ujenzi wa mifereji ya maji ya mvua – Chelsea – Lyazungu na Shunu Magobeko (Kilomita 4.9)

About The Author

error: Content is protected !!