
Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA, Mhandisi Mkama
KAIMU Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es salaam (DAWASA) Mhandisi Mkama Bwire amesema DAWASA inatambua na itashughulikia changamoto ya huduma ya maji wilaya ya Temeke ambapo bado wanatumia mitambo ya zamani pamoja na visima. Anaripoti Apaikunda Mosha. Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza katika ufunguzi wa Kikao Kazi na Wenyeviti wa Serikali za mitaa leo tarehe 20 Februari 2025, katika Wilaya ya Temeke, Mhandisi Bwire amesema DAWASA bado inaona umuhimu wa viongozi wa mitaa katika usimamizi wa karibu wa huduma za Majisafi na usafi wa Mazingira.
Amesema pia kwa kushirikiana na hao viongozi wa mtaa wenye dhamana ya wananchi, changamoto hizo za maji kwa wananchi zinaweza kutatulika kwa kiwango kikubwa sana kwa kuwa DAWASA wanatambua kuwa hali ya huduma ya maji katika wilaya ya Temeke sio nzuri, jumla ya kata 23 pamoja na mitaa142 mtandao mkubwa wa maji haujawafikia.
“Lazima tuwe na mambo ambayo tunataka kushirikiana na kujenga uelewa wa pamoja wakati tunapokwenda kuhudumia wananchi kile atakachosema Mwenyekiti basi kiwe hicho hicho atakachosema DAWASA,” amesema Bwire.
Pamoja hayo Bwire amesema atawaonyesha hali halisi ilivyo katika maeneo hayo na pia kupokea maoni ya wenyeviti ili kujenga uelewa na mikakati ya pamoja itakayosaidia kuwezesha uboreshwaji wa huduma ya maji.
Aidha, Bwire amesema kuwa anataka kuirudisha DAWASA iwe ni ya wananchi, hivyo watawezesha wenyeviti wa mitaa kutatua baadhi ya changamoto ndogo ndogo zinazoweza kutatulika, kama vile maji kumwagika, wizi wa miundombinu na changamoto za usomaji wa bili ili kurahisisha utendaji wa kazi.
ZINAZOFANANA
SBL yazindua kampeni ya SMASHED kukabiliana na unywaji wa pombe chini ya umri
Uingereza yafurahishwa na maboresho Bandari ya Dar, yaipongeza serikali
Vyombo vya dola kikwazo kwa mawakili kutimiza majukumu yao