October 23, 2024

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Wadau wa biashara kujadili mifumo ya serikali kusomana

Afisa Mtendaji Mkuu Brela, Godfrey Nyaisa.

 

WADAU zaidi ya 300 waliopo kwenye mnyororo wa urasimishaji biashara nchini, kutoka taasisi za umma, sekta binafsi, taasisi miamvuli, wafanyabiashara, wanazuoni, wajasiriamali na mawakili, wanatarajiwa kujadili fursa, changamoto na mafanikio ya mifumo ya biashara. Anaripoti Restuta James, Dar es Salaam … (endelea).

Taarifa iliyotolewa na Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (Brela), kwa vyombo vya habari leo tarehe 23 Oktoba 2024, imesema kuwa washiriki hao watajadili mada kuhusu mifumo ya taasisi za Serikali kusomana na inavyochochea uwezeshaji wa bishara nchini.

Imesema mkutano huo pia utatoa mrejesho wa maoni, ushauri na mapendekezo yaliyotolewa na wadau mwaka jana.

“Mkutano utaweka mkakati wa pamoja ili kuboresha huduma, kupata maoni juu ya utendaji kazi wa Brela hasa matumizi ya mifumo kwa kusomana na mifumo ya taasisi zingine,” imesema sehemu ya taarifa hiyo.

Imefafanua kuwa washiriki wataeleza changamoto zinazowakabili na kuzitafutia ufumbuzi, ili kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara na kukuza uelewa wa wadau kuhusu sheria, kanuni na taratibu, zinazoongoza utoaji wa huduma za usajili, ulinzi na utoaji Leseni.

“Lengo ni ili kuimarisha utekelezaji wa sheria za nchi na kujadili masuala yanayohusu maendeleo ya sekta ya biashara nchini ikiwemo fursa zinazotokana na mabadiliko ya teknolojia na namna yanavyochochea ukuaji wa biashara,” imeongeza.

Imefafanua kuwa mkutano huu, utaendeshwa kwa muundo wa mdahalo ambao utawezesha watoa mada, wachagizaji na waongoza mijadala, kuibua mjadala kulingana na mada husika.

Mkutano huo ambao utafanyika Ijumaa tarehe 25 Oktoba 2024, utaongozwa na kaulimbiu ‘mifumo ya kitaasisi inayosomana na uwezeshaji wa biashara nchini’, unakusudia kuimarisha ushirikiano baina ya Brela, sekta ya mmma na binafsi.

“Kwa kuwa urasimishaji wa biashara ni mchakato, ni vema kupitia mkutano huu sekta za umma zinazoratibu urasimishaji wa biashara nchini wakasikiliza namna bora sekta binafsi inavyopenda ihudumiwe kupitia mifumo kusomana,” imesema.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa mkutano huo ni mwendelezo wa wakala huo kukaa na wadau kila mwaka ili kubaini fursa, mafanikio na changamoto zinazoikabili sekta binafsi.

About The Author