October 17, 2024

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Urusi yapiga mikoa mitano Ukraine usiku

 

JESHI la Urusi limetumia ndege zisizo na rubani za kamikaze na shahid, katika maeneo ya Kaskazini na Kusini mwa Ukraine usiku kucha. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).

Jeshi la Anga la Ukraine, linaripoti kuwa mabomu ya shahid yalirushwa katika maeneo tofauti juu ya mikoa ya Sumy, Poltava, Cherkasy, Kherson na Nikolaev.

Kituo cha ufuatiliaji wa vita nchini Ukraine, kimeripoti kuwa tayari kuna ndege zisizokuwa na rubani 50 zilizorushwa na jeshi la Urusi katika anga ya nchi hiyo.

Matangazo ya tahadhari ya mashambulizi ya angani yametangazwa karibu eneo lote la mashariki mwa Ukraine, kufuatia mashambulizi hayo.

Wakati hayo yakijiri meya wa Kharkov na vyombo vya habari vya Ukraine, wameripoti kuwa jeshi la Urusi limeupiga mji huo kwa mabomu ya ‘glide.’

“Kharkov inashambuliwa na adui…uwe mwangalifu. Mashambulizi ya mara kwa mara yanawezekana,” Meya wa Kharkov, Igor Terekhov ameandika kwenye ukurasa wake wa Telegram.

Kwa mujibu wa Terekhov, shambulizi hilo lililenga wilaya za Shevchenkivsky na Kievsky za Kharkov, na habari kuhusu athari za mashambulizi hayo bado hazijatolewa.

Ukurasa wa Telegram wa mkuu wa utawala wa mkoa wa Kharkiv, Oleg Sinegubov, umeandika kuwa taarifa za awali zinaonesha kuna uharibifu wa miundombinu ya raia.

About The Author