September 19, 2024

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Rais Samia aacha alama ya kipekee Morogoro

 

RAIS Samia Suluhu Hassan amehitimisha ziara yake ya siku sita mkoani Morogoro huku akiacha alama kubwa kwa uzinduzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo na timu ya wanasheria waliosaidia kutoa msaada wa sheria bure kwa maelfu ya wananchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Morogoro … (endelea).

Wananchi wengi walifurahia msaada wa kisheria walioupata kutoka kwa wanasheria wa mpango wa mnsaada wa sheria wa Mama Samia Legal Aid ambao bado wanaendelea kutoa msaada kwenye viwanja vya nane nane mkoani hapa.

Kulikuwa na timu ya wanasheria kutoka Wizara ya Katiba na Sheria waliokuwa wakisikiliza kero za kisheria kwenye ziara hiyo na kuzitatua na kulikuwa na timu ingine ya Rais Samia ambayo inaendelea kutoa huduma hiyo katika maonyesho ya nane nane yanayoendelea mkoani Morogoro.

Baadhi ya wananchi wametoa ushuhuda wa namna walivyonufaika na ziara ya Rais Samia kwa huduma za msaada wa kisheria walizopata kwenye ziara hiyo.

Mmoja wa wananchi waliopata msaada wa kisheria kutoka kwa Mama Samia Legal Aid anasema amefurahia mpango huo kwani umekuw mkombozi kwa watu ambao hawana uwezo wa kuweka mawakili.

“Mpango wa Mama Samia imekuwa msaada mkubwa kwa wananchi napendekeza kama itampendeza Rais Samia hii isiwe tu kampeni maana kampeni inaisha muda ila ikiwa Taasisi ya kudumu itawasaidia sana wananchi wanyonge ambao wanapambana sana kusaka haki zao kisheria.”

Mkazi mmoja wa mkoani Morogoro Juma Hamadi ambaye akipata msaada wa kisheria nane nane alisema alisema amepata huduma kwa ukarimu wa hali ya juu kwa watumishi wa mpango wa mama Samia na anatarajia matatizo yake ya mgogoro wa shamba yatamalizika.

Anasema wananchi wengi hawana uwezo wa kuweka mawakili kusimamia kesi zao hivyo aliomba serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria kuufanya mpango huo wa msaada wa sheriaa kuwa endelevu.

Mwanaidi Selamani alisema alitembelea banda hilo la sheria la Mama Samia na amekutana na amepata ufumbuzi wa matatizo yake ya mgogoro wa nyumba ambao ulikuwepo kwa muda mrefu Kibaigwa.

“Hapa kwa msaada wa Rais Samia tunapata msaada wa kisheria bure tunamshukuru Rais Samia huyu mama anawapenda wananchi wake kwa kweli apewe maua yake hii huduma ni mkombozi kwetu,”anasema.

Mkazi wa Morogoro Mjini, Antony Gervas, yeye anasema huduma za msaada wa sheria ziwe endelevu kwani wengi hawana uwezo na kuongeza kuwa katika maonesho ya nanenane amejifunza kupitia kampeni hiyo itasaidia wananchi wengi wasiokuwa na uelewa wa kisheria kuhusu masuala mbalimbali.

“Kwa mpango huu Rais Samia anastahili kupongezwa sana na namshukuru kwa kampeni hii ambayo imepiga kambi hapa nanenane Morogoro kwasababu itawasaidia wananchi na watanzania kwa ujumla kupata haki zao,”anasema.

Naye, Ibrahim Waso mkazi wa Arusha ambaye alihudhuria maonyesho hayo Nane Nane Morogoro anasema amepata huduma nzuri kwenye banda la kampeni hiyo na amejifunza mambo ya kisheria ya kufuata na kutoa elimu kwa wananchi wenzao wa vijijini.

“Tumepewa namba za kupiga kwa ajili ya msaada wa kisheria tutawapa watendaji wasambaze kwa wananchi ili wanufaike na huduma hii ya msaada wa kisheria ya Mama Samia, tunamshukuru sana Rais hakika mama anaupiga mwingi kwa wananchi wake,”anasema.

Mkazi wa Kihonda Morogoro , Jamila Abdalah anasema amefarijika kupata huduma nzuri ambayo hakutegemea kuipa ya elimu ya masuala ya sheria.

“Nampongeza sana Rais kwa kuona umuhimu wa kampeni hii, kweli watu wengi hapa nchini hawana uwezo wa kuweka mawakili na tunajua mawakili ni ghali lakini ameliona hilo na kuleta kampeni hii ambayo itawasaidia sana watanzania tunashukuru sana,”anasema.

Kampeni hiyo hadi sasa imewafikia wananchi zaidi ya 490,000 wa mikoa saba na kutatua migogoro iliyokuwa ikiwakabili.

Kampeni hiyo inafanyika kwa miaka mitatu na ilianza mwezi Machi, 2023 hadi mwezi Februari, 2026 kwenye mikoa yote ya Tanzania Bara na Zanzibar ikilenga kuboresha upatikanaji wa haki kwa watu wasiojiweza.

About The Author