Bunge la Tanzania
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo amesema ni wakati sasa Bunge lijikite kujadili masuala makubwa ya msingi ya maendeleo badala ya kushughulikia hoja ndogondogo zinazopaswa kutatuliwa katika ngazi za serikali za mitaa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Profesa Mkumbo ameeleza kuwa haipaswi kufika hatua ambapo Bunge linajadili masuala kama ujenzi wa madarasa au matundu ya vyoo, akisisitiza kuwa mambo hayo yanapaswa kushughulikiwa na mamlaka za serikali za mitaa zilizo karibu na wananchi.
Amesema kuimarisha utendaji wa serikali za mitaa kutasaidia kushughulikia kero za wananchi kwa ufanisi zaidi, huku Bunge likibaki na jukumu la kujadili sera, mipango na masuala makubwa ya maendeleo ya taifa.
“Tunatarajia ifike mahali Bunge hili lisijadili habari ya kujenga madarasa au matundu ya vyoo. Mambo haya yafanyike kwenye serikali za mitaa — lazima tuimarishe hayo. Kero zishughulikiwe kwenye serikali za mitaa, Bunge lijadili mambo ya msingi ya maendeleo,” amesema Prof. Mkumbo.
Kauli hiyo inachochea mjadala mpana kuhusu mgawanyo wa majukumu kati ya ngazi za utawala, huku wadau wakisisitiza umuhimu wa kuongeza ufanisi katika kusimamia maendeleo ya wananchi kuanzia ngazi ya chini hadi taifa.
ZINAZOFANANA
Mahakama Kuu Z’bar yaipiga stop ZEC kuteketeza nyaraka za uchaguzi
Spika Zungu amkingia kifua mbunge aliyeshindwa kuongea kiingereza
Spika aitaka Serikali iweke maeneo ya kihistoria ya Papa Leo XIV