September 28, 2024

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Timu ya netiboli ya Maliasili yafuzu robo fainali Shimiwi

 

TIMU ya netiboli ya Wizara ya Maliasili na Utalii imeandika historia kwa kufuzu kwa mara ya kwanza hatua ya robo fainali ya Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Idara na Wizara za Serikali (SHIMIWI) yanayoendelea kufanyika Mkoani Morogoro. Anaripoti Yusuph Kayanda, Morogoro … (endelea).

Ushindi huo umepatikana baada ya timu hiyo kuibamiza timu ya TAKUKURU goli 27 kwa 20 katika mchezo uliokuwa na ushindani mkali dhidi ya mahasimu hao ambapo Wizara hiyo ilifanikiwa kuishinda timu hiyo na kuvunja mwiko wa kutokufuzu mashindano hayo tangu timu hiyo ilipoanza kushiriki michuano hiyo ya SHIMIWI hadi kufikia sasa

Akizungumza mara baada ya ushindi huo, Kocha mahiri wa timu hiyo, Rahma Kilimba, ameipongeza timu hiyo kwa kuweka historia ya kipekee ya kufuzu hatua ya robo fainali ya michuano hiyo huku akisistiza kuwa wachezaji wake wana ari ya kutosha na anaimani timu hiyo itafika fainali ya michuano na hata kuchukua ushindi katika michuano hiyo

“Ni siku ya kihistoria kwetu kufuzu robo fainali kwa mara ya kwanza. Tumefanya kazi kwa bidii na tunafurahia kufika hapa. Tunatumai kuwa tutashinda robo fainali na hatimaye kufika fainali katika michuano hii kwa sababu ari ya kufika huko tunayo,” amesema Rahma.

Kwa upande wake Mchezaji wa timu hiyo, Asha Kitungo amesema wao kama wachezaji wanaimani kubwa ya kufanya vizuri zaidi huku akitoa sifa kede kede kwa Rahma kwa kuwafunda na hatimae kufika hatua hiyo adhimu

Mratibu wa Michezo wa Wizara, Getrude Kassara ametumia fursa hiyo kuwapongeza wachezaji hao kwa kuendelea kuipeperusha Bendera ya Wizara ya Maliasli na Utalii huku akisisitiza kuwa hatua ya wao kufuzu ni jambo la kihistoria na zuri la kupongezwa

“Hongereni sana wachezaji wetu, mnaipeperusha vyema bendera ya Wizara ya Maliasili na utalii, tunawapongeza sana, hongereni kwa kuingia robo fainali, sula hili ni la kihistoria,” alisema Kassara

Aidha, ameeleza kuwa uongozi mzima wa Wizara pamoja na uongozi wa timu ya Wizara uko nyuma yao kwa kila hatua, hivyo waendelee kupambana na kuutangaza utalii kupitia michezo

Katika siku ya leo, Jumla ya michezo mitatu ya raundi ya 16 bora imechezwa kwa upande wa Wizara ambapo, Mchezo wa Netiboli na Kamba ( Me) Wizara imeibuka mshindi na kufuzu hatua ya robo fainali huku kwa upande wa Kamba (ke) Wizara hiyo ilishindwa kusonga hatua ya mbele mara baada ya kupoteza mchezo wake dhidi ya Wizara ya Afya.

About The Author