September 19, 2024

Mwanahalisi Online

Habari za Uhakika

Wakulima wa miwa Kilombero wamgeuka Mpina

 

Wakulima wa miwa katika Bonde la Mto Kilombero mkoani Morogoro wamekanusha taarifa zilizotolewa na Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina (CCM) na baadhi watu waliodanganya kuwa ni wawakilishi wa wakulima na kudai bei ya miwa imeporomoka na hawalipwi fedha zao kwa wakati. Anaripoti Mwandishi Wetu, Morogoro … (endelea).

Wakizungumza na waandishi wa habari wilayani Kilombero viongozi wa umoja wa vyama vya wakulima pamoja na baadhi ya wakulima wanaounda vyama 17 vya ushirika (AMCOS), wamekanusha taarifa hizo wakidai kuwa ni upotoshwaji unaofanywa kwa maslahi ya kisiasa.

“Hakujawahi kutokea bei ya miwa kushuka kwani tangu tuanze kuuza miwa msimu huu tumeuza kwa bei ya 108,000 tofauti na hizi taarifa za uongo zinazosambaa,” alisema Deo Msifuni.

Aidha, wakulima hao wamedai kuwa hakujawahi kutokea ucheleweshwaji wa muda mrefu wa malipo kwa wakulima kutoka kwenye kiwanda cha kuzalisha miwa na badala yake malipo yalichelewa kwa siku mbili tu kutokana na mifumo mipya iliyowekwa kiwandani hapo ambapo walitakiwa kulipwa tarehe 15 na badala yake walilipwa tarehe 17.

Wakulima hao wamesisitiza kwamba hakuna athari zozote zilizowapata kufuatia uamuzi wa serikali kutoa vibali vya kuagiza sukari nje kupunguza ongozeko la bei ya bidhaa hiyo ili kuleta ahueni kwa wananchi.

Vilevile wamesema kuwa vyama vyao vina ushirikiano mzuri na kiwanda cha sukari Kilombero na wanayo matumaini makubwa ya mageuzi ya zao hilo, kwa kuwa kiwanda hicho kinalenga kufanya upanuzi mkubwa utakaopelekea wakulima kuuza miwa kwa wingi zaidi.

About The Author