MWENYEKITI wa Bunge la Tanzania ambaye pia ni Mbunge wa Ilala, Mussa Zungu amechukua fomu ya kuwania uspika wa Bunge hilo la Tanzania. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Pia, wabunge wa Bunge hilo, Emmanuel Mwakasaka wa Tabora Mjini ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge amechukua fomu kuwania nafasi hiyo.
Wengine ni Mbunge wa Geita, Joseph Msukuma na Profesa Handley Mafyenga wamechukua fomu.
Wote hawa wamechukua leo Jumane, tarehe 11 Januari 2022, ofisi za CCM Dar es Salaam na Dodoma.
Waliochukua jana wakati dirisha lilipofunguliwa ni, Dk Saimon Ngatunga, Tumsifu Mwansamale, Melkion Ndofu, Naibu Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson, Godwin Kunambi na Ambwene Kajula, waliochukulia fomu zao Dodoma.
Waliochukulia fomu katika ofisi ndogo ya makao makuu ya CCM Dar es Salaam, ni Patrick Nkandi, Stephen Masele na Hamidu Chamani.
Wote hao wanataka kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Job Ndugai ambaye alijiuzulu tarehe 6 Januari 2022, baada ya shinikizo kutoka kwa wenyeviti wa CCM wa mikoa, wabunge na makada, kutokana na kauli yake kwamba nchi itapigwa mnada kutokana na madeni.
Ndugai alitoa kauli hiyo, wakati akizungumza kwenye mkutano mkuu wa Mikaleli ya Wanyausi wa Kabila la Wagogo, mkoani Dodoma, ambapo alikosoa utaratibu unaoendelea wa Serikali kukopa, ni mzigo usio na tija na kuitaka Serikali iachane na mikopo ya kimataifa, kwa kuwa nchi inaweza kupigwa mnada.
Alikwenda mbali pale alipotolea mfano wa mkopo kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Sh trilioni 1.3 ambazo zilizoelekezwa kutekeleza miradi ya maji, afya, utalii, elimu na ujasiriamali, huku akitaka wananchi ifikapo mwaka 2025 kuchagua mikopo au tozo.
Kutokana na uamuzi huo wa Ndugai kujiuzulu, juzi CCM kupitia kwa Katibu wa Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka ilitangaza kuanza mchakato wa kuchukua fomu za kuomba kugombea nafasi hiyo, kwa mwanachama anayetaka ambapo kwa jana pekee watatu walijitokeza.
Leave a comment