NAIBU Spika wa Bunge, Mussa Azan Zungu, amewaeleza wabunge kuwa Uchaguzi Mkuu wa 2025, uko mbioni hivyo washirikiane kutekeleza miradi ya Serikali. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Zungu ametoa kauli hiyo leo Ijumaa, tarehe 11 Februari 2022, muda mfupi baada ya Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson kumtangaza mshindi wa nafasi ya Naibu Spika wa Bunge na kumkabidhi majukumu.
Spika Tulia alimtangaza Zungu kuwa mshindi wa nafasi ya Naibu Spika wa Bunge, baada ya kupata kura za ndiyo 296 sawa na asilimia 98.35, huku akipata kura za hapana tatu kati ya kura 301 zilizopigwa. Kura zilizoharibika ni mbili.
Mbunge huyo wa Ilala kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), amesema siasa zikishatoka kwenye uchaguzi zinarudi bungeni na kuwa wabunge wanapaswa kuhakikisha pesa zinazotolewa na Serikali kutekeleza miradi hiyo zinatumika ipasavyo kwenye halmashauri za maeneo yao.
“Uchaguzi wa 2025 is chassing around the corner (unafukuzia kwenye kona), siasa zikishatoka kwenye uchaguzi zinarudi bungeni na bungeni ni kushirikiana na miradi ya Serikali, kuhakikisha pesa zinazotolewa na Serikali zinasimamiwa vizuri kwenye halmahsuri zetu,” amesema Zungu.
Aidha, Zungu ameahidi kushirikiana na wabunge kulijenga Taifa, huku akiwapongeza kwa kusimamia ujenzi wa madarasa ya shule za Sekondari, uliotekelezwa kupitia fedha za kukabiliana na athari za Ugonjwa wa Virusi vya Korona (UVIKO-19), kutoka Shirika la Fedha za Kimataifa (IMF).
“Niwapongeze wabunge wote walioshiriki kwenye kujenga madarasa na kujenga heshima ya Taifa letu , kuwaingiza watoto 150,00 kwa mpigo kwenye kidato cha kwanza. Namshukuru Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, kwa kazi uliyofanya na mawaziri wako, waziri wa fedha, Dk. Mwigulu Nchemba aliyeenda kusaidiana na Rais Samia Suluhu Hassan, kutafuta fedha,” amesema Zungu.
Awali wakati akiomba kura za wabunge, Zungu aliahidi kuwa, atatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Kanuni za Bunge, toleo la 2020, chini ya maelekezo ya Spika Tulia.
Zungu anachukua nafasi ya Dk. Tulia, aliyoiacha wazi baada ya kugombea na kuchaguliwa kuwa Spika, kufuatia hatua ya Job Ndugai kujiuzulu kushika wadhifa huo.
Leave a comment