MUSSA Azzan Zungu, Mbunge wa Ilala amesema licha ya manispaa hiyo kupandishwa kuwa Jiji, kuna barabara mbovu. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza kwenye ziara ya Rais Magufuli Magufuli katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam leo tarehe 25 Februari 2021, Zungu amemwomba Rais Mgufuli kukumbuka kuelekeza ujenzi wa barabara kupitia mradi wa maendeleo namba mbili wa DMDP.
Katika siku yake ya pili ya ziara, leo Rais Magufuli amezindua Soko Kuu la Kisutu na jengo la Uhuru Media ambalo linabeba vyombo vya habari vya Uhuru ikiwa ni pamoja na Classic FM, Channel ten, Channel ten Plus na Magic FM.
Kwenye mkutano huo Zungu amesema, msingi wa kuomba kukumbukwa kwenye mradi huo, ni kutokana na Ilala ambayo sasa ni jiji lenye majimbo matatu (Ilala, Segerea na Ukonga), kuwa na miundombinu isiyo rafiki na inayosababisha adha wakati wa mvua.
“Pamoja na kupandisha Manispaa ya Ilala kuwa Jiji, tunazo changamoto. Tunayo majimbo matatu Ilala, Segerea na Ukonga. Miundombinu yetu bado iki chini.
“Kuna maeneo inapopatikana mvua, majimbo yote matatu shida kubwa sana, nikuombe mheshimiwa rais, kwa unyenyekevu mkubwa sana, Mungu akutie imani miradi hii ya DMDP namba 2 ambayo yapo katika mazungumzo na ya serikali na wafadhili, utusaidie kutupatia barabara,” amesema Zungu.
Amefafanua, kwamba mpaka sasa Ilala pamoja na kuwa jiji, licha ya kuwa katikati lakini kuna barabara mbovu na zingine lami isiyoridhisha.
“Katika jimbo hili (Ilala), mtandao wa barabara ni kilomita 133, katika hizo kilomita 55 ni za lami ambazo zinaridhisha lakini kilomita 17 ni za lami mbaya.
“Kuna kilomita 7.2 ambazo ni za lami mpya kwa ufadhili wa tarura na kilomita 52 ni vumbi ndani ya center (katikati) ya halmashauri mpya ya Jiji la Dar es Salaam,” amesema.
Amesema, Ilala ndio mjini na ndio mapato mengi yanapatikana, kwamba biashara nyingi maeneo ya mjini zimekufa kwasababu wafanyabiashara wengi na wateja wao, waliona wasiende ,jijini kwa sababu miundombinu sio mizuri.
“Nikuahidi, mradi umetupa hii halmashauri mpya vyanzo vyetu, nikuahidi na miundombinu ikiboreka, ujenge tu barabara, unawekeza mapato makubwa ya serikali yako,” amesema.
Leave a comment