KIONGOZI wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe, amekanusha tuhuma za kwamba yeye ni msaliti wa kisiasa, akisema angekuwa msaliti asingechaguliwa kuwa mbunge zaidi ya mara tatu pamoja na kupewa dhamana ya kukiongoza chama chake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Zitto amekanusha madai hayo katika mahojiano yake na Kituo cha Runinga cha ITV, kupitia kipindi cha Dakika 45, kilichorushwa jana Jumatatu, baada ya kuulizwa ana kauli gani kuhusu tuhuma za usaliti zilizoibuliwa dhidi yake.
“Kuna watu wana mitizamo pia, huwezi kuzuia. Mimi sio msaliti, mimi ni mwanasiasa naaminika kisisasa ndiyo maana nimechaguliwa na wananchi wa Kigoma zaidi ya mara tatu tena majimbo tofauti, ndiyo maana nimechaguliwa na wenzangu kufanya siasa ishara moja kubwa ya kuaminika. Huwezi kuwa mwanasiasa kila mtu akiwa anakupenda, utakuwa mwanasiasa gani wewe?” alisema Zitto.
Zitto alisema “wapo watu ambao wananiona kwa jicho hilo tofauti, Zitto ni kiongozi wa kisiasa ambaye anaamini katika msimamo fulani ya kisiasa. Muda wote nimekuwa mstari wa mbele na mnaona namna ambavyo tunajenga chama katikati kabisa ya kukata tamaa lakini huioni ACT-Wazalendo ikikata tamaa , inajipangusa inasonga mbele.”
Mwanasiasa huyo alisema kuwa, hata chama chake kinaaminika ndio maana ACT-Wazalendo inaendelea kukua kwa kasi kutokana na kutetea maslahi ya wananchi hasa wakulima, wafugaji na wafanyabiashara.
Tuhuma za usaliti dhidi ya Zitto ziliibuliwa na baadhi ya wanachama wa vyama vingine vya upinzani, kufuatia hatua ya chama chake kushiriki katika masuala ambayo vyama vingine vimesusia kushiriki, ikiwemo kushiriki chaguzi za marudio, kushiriki mchakato wa ukusanyaji maoni ya kuboresha mfumo wa demokrasia ya vyama vingi uliofanywa na Kikosi Kazi cha Rais Samia Suluhu Hassan.
Asante ndugu zitto kweli kabisa wewe sio msaliti isipokuwa umezidi kuwa na tamaa ya madaraka kumbuka ulifukuzwa chadema kwa tamaa ya madaraka