MAALIM Seif Sharif Hamad, Mshauri Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo anatarajia mwelekeo mpya wa vyama vya upinzani nchini baada ya Zitto Kabwe na Tundu Lissu kukutana na kuzungumzia namna ya ushirikiano. Anaripoti Martin Kamote … (endelea).
Zitto ambaye ni Kiongozi Mkuu wa ACT-Wazalendo, alikwenda kumjulia hali Lissu nchini Ubelgiji anakopatiwa matibabu baada ya kushambuliwa kwa risasi jijini Dodoma ‘Area D’ tarehe 7 Septemba 2019.
Lissu ambaye ni Mwanasheria Mkuu wa Chadema na aliyekuwa mbunge wa jimbo la Singida Mashariki, alikutana na Zitto na kufanya mazungumzo yanayolenga namna ya kushirikiana kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa na uchaguzi mkuu mwakani.
Kupitia ukurasa wake wa Twitter tarehe 3 Septemba 2019, Maalim Seif ameandika kuwa Zitto na Lissu wameleta faraja kwa wadau wa siasa hasa za upinzani kwa kuonesha njia kuelekea 2020.
Maalim Seif amewapongeza wanasiasa hao kwa hatua hiyo, na kuwataka wazidi kushirikiana kwa pamoja katika kubadilisha historia ya Tanzania kupitia uchaguzi wa 2020.
Mwanasiasa huyo mkongwe hapa nchini, ameeleza kwamba uchaguzi huo nimuhimu kuliko chaguzi zote katika kuamua mustakabali wa Tanzania.
Ameandika “Zitto Kabwe na Tundu Lissu wametupa faraja na kutuonesha njia kuelekea 2020. Nawapongeza na kuwatia moyo kutekeleza wajibu wa kihistoria kwa Tanzania wakati tunaelekea uchaguzi mkuu wa 2020 ambao ni uchaguzi muhimu kuliko chaguzi zote katika kuamua mustakbali wa Tanzania.”
Leave a comment