KIONGOZI wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe, amemshauri Rais Mteule wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), Dk. Edward Hoseah, kuwaunganisha mawakili wa chama hicho katika kutetea utawala wa sheria nchini. Anaripoti Regina Mkonde, Arusha … (endelea).
Zitto ametoa ushuri huo Ijumaa tarehe 16 Aprili 2021, kupitia ukurasa wake wa Twitter, saa kadhaa kupita baada ya Dk. Hoseah kutangazwa mshindi wa kiti cha Urais wa TLS katika Uchaguzi Mkuu wa chama hicho.
Kwenye uchaguzi huo, uliofanyika leo Ijumaa katika viwanja vya Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC), jijini Arusha, Dk. Hoseah alichuana na Flaviana Charles, Shehzada Walli, Albert Msando na Francis Stolla.
Natoa pongezi zangu kwa Mwanasheria Edward Hosea kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika @TanganyikaLaw na kwa Wanachama wote wa TLS kwa kumaliza Uchaguzi salama. Tunataraji Dkt Hosea atajitajidi kuwaunganisha wanasheria wote katika kutetea utawala wa Sheria
— Zitto MwamiRuyagwa Kabwe (@zittokabwe) April 16, 2021
“Natoa pongezi zangu kwa Mwanasheria Edward Hoseah, kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa TLS na kwa wanachma wote wa TLS kwa kumaliza uchaguzi salama.”
“Tunataraji Dk. Hoseah atajitahidi kuwaunganisha wanasheria wote katika kutetea utawala wa sheria,” amesema Zitto
Naye Rais Mstaafu wa TLS, Wakili Fatma Karume, amesema, uchaguzi huo ulikuwa huru na wa haki, huku akimpongeza Dk. Hoseah kwa kuchaguliwa kuwa rais wa chama hicho kwa mwaka 2021/2022.
“Ni uchaguzi pekee ulio huru na wa haki Tanzania. Rais wa TLS 2021-2022 ni Dk. Hoseah. Pongezi kwake,” ameandika Fatma katika ukurasa wake wa Twitter.
The only FREE and FAIR election in #Tanzania. The TLS President 2021-2022 is Edward Hoseah.
Well done to him. https://t.co/bf2TerLmGc— fatma karume aka Shangazi (@fatma_karume) April 16, 2021
Kwa mujibu wa matokeo yaliyotangazwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya TLS, Charles Rwechungura, Dk. Hoseah ameshinda kiti hicho baada ya kupata kura 293 kati ya 802 zilizopigwa.
Aliyeshika nafasi ya pili ni Flaviana, aliyepata kura 223, huku wa tatu akiwa Walli (192), wakati Msando akishika nafasi ya nne (69). Stolla alifunga dimba kwa kupata kura 17.
Kesho Jumamosi tarehe 17 Aprili 2021, Dk. Hoseah ataapishwa kuchukua mikoba ya Dk. Rugemeleza Nshala, aliyemaliza muda wake wa uongozi.
Leave a comment