ZITTO Kabwe, Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), amelitaka Jeshi la Polisi Tanzania kutoa taarifa ya kina kuhusu tukio la mapigano kati ya askari na wananchi jamii ya Wanyantuzu wilayani Uvinza mkoani Kigoma. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Tukio hilo lililotokea takribani siku 10 zilizopita, ambapo inadaiwa askari wawili kufariki dunia huku idadi ya wananchi waliopoteza maisha ikiwa haijulikani.
Kiongozi huyo ameetoa kauli hiyo leo Jumapili Oktoba 28, 2018 katika mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika kwenye ofisi za makao makuu ya chama hicho Kijitonyama, Dar es Salaam.
Zitto ameomba idadi ya waliopoteza maisha katika tukio hilo kuwekwa wazi.
“Viongozi walikwenda eneo la tukio tunataka waseme, si tu kupata taarifa ya polisi bali tupate na sauti za wananchi juu ya kitu kilichotokea huko,” amesema Zitto.
“Tunahitaji kupata taarifa kamili ni wangapi walijeruhiwa, waliopoteza maisha kwa sababu wale ni Watanzania na wana haki ya kupewa ulinzi na kuishi sehemu yoyote.”
Amesema kama walifanya makosa kwa kuvamia eneo ambalo halitakiwi kufanyika shughuli za binadamu kuna taratibu za kufuata na si watu kuuawa.
“Vyombo vya habari havitoi taarifa kwa sababu wenye taarifa hawazitoi kwa wanahabari. Jana tulipata taarifa watu wanne walikwenda kupatiwa matibabu katika kituo cha afya cha Nguruka jambo hili ni baya na linatakiwa kukemewa,” amesema.
Leave a comment