MAHAKAMA ya Hakim Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, imempa dhamana mwanasiasa machachari wa upinzani nchini, Zitto Zuberi Kabwe. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Zitto aliyefikishwa mahakamani hapo mchana wa leo, ameshitakiwa kwa makosa matatu, likiwamo suala la “uchochezi” kuhusiana na madai ya mauwaji ya wananchi katika kijiji cha Mpeta, wilayani Uvinza. Alikana mashitaka hayo.
Awali mwendesha mashitaka wa serikali aliwasilisha hati ya kiapo ya kutaka mahakama kumnyima dhamana mshitakiwa kwa madai kuwa kuwa kwake nje “kutahatarisha usalama wake.”
Akitoa uamuzi wa pingamizi hilo la dhamana, Hakimu anayesikiliza shauri hilo amesema, “dhamana ni haki ya mshitakiwa na kwamba jukumu la ulinzi wa raia, liko mikononi mwa polisi.”
Mbunge huyo wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), alifikishwa katika Mahakama ya Kisutu, leo Ijumaa, tarehe . Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Zitto ambaye alikamatwa akiwa nyumbani kwake, maeneo ya Masaki, anashikiliwa na jeshi la polisi tangu juzi Jumatano, kwa madai ya “uchochezi.”
Anatuhumiwa kutoa taarifa za uongo kuhusu mauaji ya baadhi ya askari polisi na wananchi katika kijiji cha Mpeta, wilayani Uvinza mkoa wa Kigoma.
Zitto, mmoja wa wanasiasa wenye ushawishi mkubwa nchini, mara baada ya kukamatwa alipelekwa kwenye Kituo cha polisi cha Oysterbay, kabla ya kuhamishiwa polisi kati na baadaye kulazwa kwenye kituo cha polisi Mburahati.
Kupatikana kwa taarifa kuwa Zitto amefikishwa mahakamani, kumekuja saa chache baada ya shirika la kutetea haki za binadamu ulimwenguni – Amnesty International – kuingilia kati kwa kulitaka jeshi la polisi kumpa dhamana mtuhumiwa au kumfikisha mahakamani.
Katika taarifa yake, Amnesty limesema, ni wajibu wa vyombo vya dola nchini kumfungulia mashtaka mahakamani Zitto au kumuachia huru mara moja.
Kabla ya kukamatwa na Polisi, Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Kigoma, Martin Ottieno, alimtaka Zitto kuwasilisha alichokiita, “vielelezo vya madai yake,” kuwa watu zaidi ya 100 wameuwa katika eneo la Uvinza.
Zitto ambaye ambaye pia ni Kiongozi Mkuu wa chama cha ACT- Wazalendo, aliwaambia waandishi wa habari wiki iliyopita kuwa wananchi zaidi ya 100 wamepoteza maisha katika vurugu zilizoibuka kufuatia mgogoro wa ardhi wilayani Uvinza.
Leave a comment