ZITTO Kabwe, Kiongozi Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo, amekutwa na kesi ya kujibu. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Umauzi huo umetolewa leo tarehe 18 Februari 2020, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kwenye kesi ya uchochezi No. Na.237 ya mwaka 2018.
Uamuzi huo umetolewa na Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi baada ya kupitia ushahidi uliwasilisha na upande wa mashtaka mahakamani hapo.
Hakimu Shaidi amesema, ipo haja ya kusikia utetezi wa Zitto juu ya tuhuma za uchochezi alizoshtakiwa kwenye mahakama hiyo.
Zitto ameieleza mahakama hiyo, kuwa atajitetea kwa njia ya kiapo na atakuwa na mashahidi 10.
Hakimu Shaidi ameahirisha shauri hilo ambapo litasikilizwa mfululizo kuanzia tarehe 17, 18, 19.
Awali, kabla ya Hakimu Shaidi kutoa uamuzi huo, upande wa mashtaka umemtaka Zitto kuieleza mahakama sababu za kutohudhuria mahakamani hapo tarehe 10 Februari 2020.
Zitto alieleza mahakama hiyo, kuwa hakuhudhuria mahakamani siku hiyo kwani aliumwa akiwa nchini Marekani, na aliwasilisha chati cha matibabu kwenye mahakama hiyo kama kielelezo .
Wakili wa Jamuhuri, Tumain Kweka amedai kuwa cheti hicho hakina uthibitisho wa kuwa aliumwa, na kwamba hakina stempu ya hospitali ambayo Zitto alidaiwa kutibiwa.
Zitto ameieleza mahakama hiyo, kuwa hana sababu za kutohudhuria mahakamani hapo ikiwa yeye ni mbunge na kiongozi mwenye dhamana kwa wananchi.
Hakimu Shaidi amesema, kwa kuwa mshtakiwa amehudhuria mahakama bila kukamatwa, hana sababu ya kufutiwa dhamana “tumuonye awe anahudhuria kesi yake kama sheria inavyoteka.”
Zitto anakabiliwa na mashtaka matatu ikiwemo kutoa maneno ya uchochezi.
Leave a comment