ZITTO Kabwe, Kiongozi Mkuu wa Chama cha ACT- Wazalendo, amekula kiapo kizito kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2020. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Amesema, chama hicho hakitakubali uchaguzi mkuu wa mwaka 2020, kunajisiwa kama ilivyokuwa kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa, uliofanyika tarehe 29 Desemba 2019.
Akifungua uchaguzi wa ndani wa chama hicho katika Jimbo la Temeke leo tarehe 29 Desemba 2019, amesema wananchi wana hasira kwa kunyang’anywa haki yao ya kuchagua viongozi wa serilikali za mitaa.
“Chama hiki hakitakubali kuingia kwenye uchuguzi mkuu wa mwaka 2020, mpaka kikomeshe vitendo vya kuhujumu uchaguzi.
“Mchezo walioufanya kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa, ndio huo huo watakaoufanya kwenye uchaguzi mkuu iwapo hatutachukua hatua stahiki zitakazowaumiza,” amesema Zitto.
Amesema, vyama vya upinzani lazima vitoe somo “lazima tutoe somo kwa watawala juu ya kuwapa haki wananchi.”
Kiongozi huyo ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Kigoma Mjini, amewambie viongozi watakaochaguliwa kwenye uchaguzi huo, kuwa tayari kuyakabili mazingira ya sasa ya siasa nchini
“Mazingira yetu ya kisiasa kwa sasa ni mabaya, mnapaswa kuwa tayari kuyakabili,” amesema.
Leave a comment