CHAMA cha ACT-Wazalendo kimeanza kueleza mikakati yake, iwapo kitapewa mamlaka ya kuiongoza Tanzania baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Zitto Kabwe, Kiongozi wa ACT-Wazalendo na Mbunge wa Kigoma Mjini amesema, serikali itakayoongozwa na chama hicho itaweka mfumo wa kodi unaoeleweka na usio kandamizi.
Na kwamba, mfumo uliopo chini ya serikali ya sasa, unamfanya mkulima kubaki mnyonge na mashine ya kuzalisha utajiri kwa watu wengine huku wao wakiendelea kuwa masikini.
Ametoa kauli hiyo leo tarehe 8 Agosti 2019, wakati akizungumza na wafanyabishara wa soko la Tandale, Dar es Salaam ikiwa ni siku ya Maadhimisho ya Siku ya Wakulima – Nanenane.
Ameeleza kushangazwa na tabia iliyojengeka sasa ambapo, sikukuu za namna hii zimegeuzwa na kuwa maeneo ambayo watawala kujikusanya kwenye mji fulani na kutoa ‘mahubiri’ yao.
Na kuwa, mahubiri yao wanayoyaona kuwa ni mafanikio na fursa ya sekta ya kilimo nchini, hayagusi kiini cha hali duni ya sekta ya kilimo nchini na namna ya kuleta mageuzi kwenye sekta hiyo nyeti.
“Kwa mazingira ya nchi kama Tanzania, kilimo ndio roho ya uchumi wa nchi. Ndio maaana, kwenye ilani yetu ya uchaguzi ya Mwaka 2015, tuliweka bayana kuwa kilimo kitakuwa ndio shughuli kiongozi katika kutokomeza umasikini na kuleta mageuzi ya kiuchumi nchini.
“Mpango wa pili wa maendeleo ya taifa umeainisha nafasi ya sekta ya kilimo katika uchumi wa Tanzania. Sekta ya kilimo inaajiri asilimia 67 ya nguvu kazi ya Watanzania. Hii ni sawa na Watanzania watu wazima milioni 18,” amesema.
Zitto amesema, sekta ya kilimo inachangia asilimia 30 ya pato la Taifa (GDP), “hii maana yake ni kuwa shughuli za kilimo zina thamani ya shilingi trilioni 38 katika pato la Taifa la shilingi trilioni 129 na sekta hiyo inaingiza Dola za Marekani 1.2 bilioni.”
Amesema, katika kipindi cha miaka minne sasa, uchumi wa mkulima ‘umesagwasagwa’ kufuatia uamuzi ya serikali kuua kilimo cha Korosho, Tumbaku, Pamba, Karafuu, Mbaazi.
“Serikali itakayoundwa na Chama cha ACT Wazalendo itatambua kuwa kilimo ndio shughuli kiongozi katika kutokomeza umasikini nchini.
“Shughuli za kilimo lazima ziendeshwe na wananchi wenyewe kwa kuwawezesha kumiliki ardhi, kuongeza tija na hivyo uzalishaji na kupata mitaji,” amesema.
Maadhimisho ya Nanenane kitaifa yamefanyika mkoani Simiyu ambapo mgeni rasmi ni Kasim Majaliwa, Waziri Mkuu.
Leave a comment