WAFUASI wa chama cha upinzani nchini Zimbabwe (MDC) wameingia barabarani kwa maandamano baada ya kukishtumu chama tawala Zanu- PF kuingilia uchaguzi huo kwa kuiba kura za ubunge na urais. Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Katika ghasia hiyo watu watatu waliripotiwa kupoteza maisha na wengine kujeruhiwa baada ya vikosi vya Usalama vilipojaribu kutuliza vurugu hizo za wafuasi wa MDC, chini ya kiongozi wao mkuu Nelson Chamisa ambaye yupo kwenye mchuano mkali na Emmerson Mnangawa wa Zanu- PF.
Jeshi la nchi hiyo leo limeonekana likipiga doria katika miji tofauti huku likiwataka wananchi wa nchi hiyo kuwa na nidhamu wakati wakiwa wanasubiri matokeo ya urais huku hali hiyo ikionekana kuzua hofu miongoni mwa wafanya biashara mpaka kufikia hatua ya kufunga maduka.
Baada ya kutokea vurugu hizo umoja wa mataifa (UN) kupitia Katibu Mkuu wake Antonio Guterres amesema serikali nchini humo inatakiwa kuhakikisha kuwa vurugu hizo hazitokei mpaka kusababaisha polisi kufyatua risasi kwa wandamanaji.
Mpaka kufikia siku ya jana Zanu-PF ambayo inaongozwa na Rais wa sasa wa nchi hiyo Emmerson Mnangawa ambaye pia ni mgombea kwenye kinyang’anyiro hicho inaonekana kuongoza kwa wingi wa viti katika nafasi ya Ubunge baada ya matokeo ya awali kutangazwa na tume ya taifa ya uchaguzi ya nchi hiyo.
Uchaguzi huo unakuwa ni wa kwanza nchini Zimbabwe tangu Rais wa muda mrefu Robert Mugabe kuondolewa madarakani na jeshi.
Leave a comment