SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), imetangaza rasmi kwamba shamba la Razaba lilipo eneo la Bagamoyo, mkoani Pwani, ni mali halali ya serikali hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Shamba hilo ambalo liko katika eneo ambalo lilikuwa likitumiwa kama ranchi ya Zanzibar Bagamoyo (RAZABA), lililopo kijiji cha Winde kata ya Makulunge.
Katika taarifa yake kwa umma, serikali ya Zanzibar, kupitia kwa msemaji wake, Charles Hilary, imeeleza kuwa shamba hilo ni mali ya serikali na haitambui mtu yoyote aliyemilikishwa; na au kujimilikisha eneo hilo.
Kwa mujibu wa msemaji huyo wa serikali Visiwani, “eneo la shamba la Makurunge, Razaba, lililopo wilaya ya Bagamoyo, kata ya Makurunge, lenye ukubwa wa takribani hekta elfu sita, ni mali ya Serikali ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, tangu mwaka 1977.”
Aliongeza: “Hivyo ni marufuku kwa mtu, taasisi au kikundi chochote, kufanya shughuli yoyote katika eneo hilo. Hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya mtu au kikundi cha watu, kitakachokwenda kinyume na tangazo hilo.”
Aidha, taarifa hiyo inasema, “serikali haitakuwa na wajibu wa kulipa fidia kwa mtu yoyote aliyepatiwa eneo katika shamba hilo.”
Mgogoro kati wananchi wa kijiji cha Winde na Ranchi ya Razaba, umedumu kwa zaidi ya miaka 40 sasa, kufuatia baadhi yao kudai kuwa eneo lao lilichukuliwa na Serikali ya Zanzibar, bila ridhaa yao na bila kulipwa fidia.
Lakini Razaba wanadai kuwa kabla ya kulichukua eneo hilo, ambalo lilikuwa likitumika kwa ajili ya kufungia ng’ombe kabla ya kusafirishwa Zanzibar, walilipa mamilioni ya fedha kama fidia kwa wananchi hao.
Ranchi ya RAZABA ilianzishwa Oktoba mwaka 1977 kwa makubaliano ya pande mbili kati ya serikali ya Zanzibar na serikali ya Jamhuri ya Muungano, ambapo jumla ya hekari 77,663 zilikabidhiwa kwa serikali ya Visiwani, kupitia iliyokuwa wizara ya kilimo na maliasili.
Wachambuzi wa masuala ya kisiasa wanasema, hatua ya serikali kung’ang’ania eneo hilo ililolitelekeza kwa takribani miaka 20 sasa, tayari imesababishia wananchi taharuki na chuki dhidi ya serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Sheria za Ardhi za Tanzania, zinatoa mamlaka ya mwisho kuhusu ardhi iliyopo Tanganyika, kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Leave a comment