KLABU ya Soka ya Yanga imesikitishwa na kushtushwa na tukio la kushikiliwa na kuhojiwa kwa mshauli wao mkuu, Senzo Masingiza jana kwenye kituo cha polisi cha Oysterbay jijini Dar es Salaam kwa tuhuma za kupanga matokeo na kuihujumu klabu ya Simba kwenye baadhi ya michezo ya Ligi Kuu. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Senzo ambaye alikuwa mtendaji mkuu wa klabu ya Simba alishikiliwa na kufanyiwa mahojiano jana kwenye kituo hicho cha polisi kwa kutuhumiwa kufanya mawasiliano yenye nia ya kuihujumu klabu ya Simba na aliyekuwa mkurugenzi wa wanachama wa klabu hiyo Hashim Mbaga.
Taarifa kutoka ndani ya klabu ya Yanga imeeleza kuwa wanapinga vikali propaganda hizo zinazoenezwa ambao siyo za kiungwana huku wakiamini kuwa mambo ya mpira wa miguu humalizwa na taasisi usika.
Aidha MwanaHALISI Online ilimtafuta Kamanda wa Polisi mkoa wa Kinondoni, Emmanuel Bukombe, kutaka kujua sababu za kushikiliwa kwa Senzo, alisema bado hana taarifa za kushikiliwa kwake kwa kuwa jana hakuwepo ofisini.
“Hilo swala sijalifuatilia bado na kujua wamemuhoji kuhusu nini, kutokana na kutokuwepo kwangu jana,” alisema Kamanda huyo.
Ikumbukwe Senzo ambye ni raia wa Afrika Kusini alijiuzulu kwenye nafasi ya utendaji mkuu kwenye klabu ya Simba tarehe 9 Agosti, 2020 na kuibukia upande wa pili ndani ya klabu ya Yanga na kuwa mshauri mkuu wa timu hiyo.
Mara baada ya hapo jana kutoka kwenye kituo cha polisi cha Oysterbay kwenye mahojiano kupitia kurasa zake za kwenye mitandao ya kijamii Senzio aliandika kuwa.
“Soka kamwe halilali, sijwahi kuwaza kwamba kutoka wekundu kwenda Yanga itasababisha UHASAMA mkubwa. Sasa ni dhahiri kwamba nimesababisha chuki na maumivu kwenye undugu wa soka la Tanzania kiasi kwamba “Watu”wanahatarisha kuchafua jina langu katika harakati za kulipa kisasi. Niko salamasalimini, niko nyumbani na najielekeza kuihudumia timu ya wananchi. Ahsanteni sana Wananchi wenzangu, tupo pamoja,” aliandika Senzo kwenye ukurasa wake wa Instagram.
Tuhuma hizi zimekuja kufuatia matokeo ya hivi karibuni ya klabu ya Simba kwenye michezo ya Ligi Kuu Tanzania Bara mara baada ya kupoteza michezo miwili mfululizo kwa kufungwa na Tanzania Prison na Ruvu Shooting.
mtimatuku@gmail.com.