VIJANA wa Jangwani jijini Dar es Salaam, Yanga wameendelea kuwapa furaha mashabiki wake, baada ya kuwadunda 2-1 maafande wa magereza, Tanzania Prisons. Anaripoti Mwandishi Wetu, Sumbawanga … (endelea).
Yanga leo Jumapili, tarehe 19 Desemba 2021, katika Uwanja wa Nelson Mandela, Sumbawanga mkoani Rukwa, wameendeleza rekodi yao ya kutopeteza mchezo wowote wa Ligi Kuu Tanzania Bara 2021/22.
Ulikuwa mchezo wa kasi na kushambuliana kwa zamu ambapo Prisons walikuwa wa kwanza kuliona lango la Yanga dakika ya 12 kupitia kwa Bangula.
Bangula aliunganisha mpira wa kona na kuwaacha mabeki wa Yanga wakishangaa pamoja na kipa wao wasijue la kufanya.
Hata hivyo, uongozi wa goli hilo, ulidumu kwa dakika kumi kwani dakika ya 23, kiungo makini wa Yanga, Feisal Salum ‘Fei Toto’ akisawazisha kwa shuti kali la mguu wa kushoto nje ya 18.
Wakionesha wanakusudia kurejesha kikombe la ligi kuu Tanzania Bara walichokikosa kwa misimu minne mfululizo kwa watani zao Simba kuchukua, kiungo mkabaji raina wa Uganda, Khalid Aucho aliifungia Yanga bao la pili dakika ya 43.
Aucho aliufunga bao hilo kwa kichwa cha kuchumpa akiunganisha basi ya Said Thibazonkiza.
Ushindi huo umewafanya Yanga kujichimbia kileleni mwa ligi hiyo kwa kufikisha pointi 23 baada ya kushuka dimbani mara tisa. Watani zao Simba iko nafasi ya pili ikiwa na pointi 18 baada ya kucheza michezo nane.
Kocha wa Prisons, Shaban Kazumba amesema, ulikuwa mchezo mzuri “na tumefungwa kwa makosa madogo tuliyoyafanya ndiyo yametuadhibu.”
“Tunajilaumu kwa nini tumepoteza mchezo huu kwani tulikuwa na uwezo wa kushinda. Tumetengeneza nafasi tumeshindwa kuzitumia,” amesema
Kwa upande wake, Kocha wa Yanga, Mohamed Nabi amesema, tulijua itakuwa mechi ngumu “na ugumu uliongozeka kutokana na ugonjwa kwa baadhi ya wachezaji. Tunawashukuru wachezaji wetu kwa kujitoa licha ya kuumwa.”
“Wamejitolea kwani licha ya kuumwa, wameamuka na kuja kucheza kwa ajili ya kuwapa moyo mashabiki wao. Kikubwa ni kuipigania nembo ya Yanga. Tunawapongeza sana wachezaji kwani wao ndiyo wanaoamua mchezo,” amesema Nabi.
Leave a comment