MCHEZO wa Ligi Kuu Tanzania Bara kati ya Yanga dhidi ya Dodoma Jiji FC utachezwa kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, jijini Arusha kutokana na wenyeji hao kuhamishia mchezo huo huko. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Yanga ambao jana waliibuka na ushindi wa mba0 2-1, dhidi ya Ruvu Shooting kutoka mkoani Pwani na kuendelea kujikita juu kwenye msimamo wa Ligi mara baada ya kukusanya pointi 34 baada ya kucheza michezo 14.
Mabao ya Yanga kwenye mchezo huo yalifungwa Michael Sarpong dakika ya 32 na bao la kujifunga la Cassian Ponela dakika ya 66 huku bao pekee la Ruvu Shooting kwenye mchezo lilifungwa na David Richard dakika ya 60.
Akijibu swali mbele ya waandishi wa habari mara baada ya mchezo huo kukamilika Afisa Habari wa klabu ya Yanga, Hassan Bumbuli alisema kuwa sababu ya mchezo huo kati ya Yanga na Dodoma Jiji kuchezwa Arusha ni kutokana na kanuni za Ligi kuu kuruhusu timu yoyote inayoshiriki Ligi hiyo kubadilisha mechi mbili kwenye msimu wa ligi kucheza katika mikoa ambayo hakuna timu ya Ligi Kuu.
“Kanuni zinaturuhusu na sisi tumeamua tutumie nafasi hiyo kwenda mkoani Arusha ambapo mara ya mwisho kuishuhudia Yanga ikicheza mchezo wa Ligi Kuu ilikuwa miaka minne iliyopita dhidi ya JKT Oljolo na tumeamua kwenda huko kutokana na siku nyingi watu hawajatuona,” alisema Bumbuli.
Kabla ya mchezo huo Yanga itamenyana na Mwadui FC kutoka mkoani Shinyanga kwenye mchezo wa Ligi Kuu utakaochezwa kwenye uwanja wa CCM Kambarage.
Mpaka sasa Yanga imebakisha michezo mitatu kukamilisha mzunguko wa kwanza wa Ligi hiyo kwenye msimu wa 2020/21, huku ikiwa timu pekee ambayo haijapoteza mchezo.
Leave a comment