KLABU ya soka ya Yanga imefanikiwa kufunga mwaka 2021 kwa kishindo mara baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 4-0, dhidi ya Dodoma Jiji FC kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea)
Mchezo huo ulipigwa hii leo tarehe 31 Desemba, 2021 kwenye dimba la Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam majira ya saa 1 usiku.
Kwenye mchezo huo ambao Yanga walitawala mpira kwa asilimia kubwa walifanikiwa kuandika bao lao la kwanza kupitia kwa Fiston Mayele kwenye dakika ya 42, na kufanya bao hilo kudumu hadi mapumziko.
Kipindi cha pili kiliporejea Yanga ilionekana kuimalika zaidi ya Dodoma Jiji na kufanikiwa kuandika bao la pili kwenye dakika ya 56 kupitia kwa Jesus Moloko mara baada ya kuunganisha mpira mrefu uliopigwa na mlinzi wao wa kati Yanick Bangala.
Mara baada ya kupata bao hilo Yanga haikuishia hapo, iliendelea kupeleka mashambulizi kwenye lango kiasi cha kupelekea mlizni wa Dodoma Jiji Justine kujifunga bao kwenye dakika ya 71 baada ya kuugusa mpira uliopigwa na Feisal Salum.
Kalamu ya mabao kwa upande wa Yanga kwenye mchezo huo ilitamatishwa na Khalid Aucho ambaye alimpigilia msumari wa bao la nne dakika ya 81.
Kwa matokeo hayo Yanga inaendelea kujikita kileleni ikiwa na alama 29, huku nafasi ya pili ikishikwa na Simba wenye alama 21 baada ya kucheza michezo tisa.
Ligi kuu hiyo itaendelea kesho kwa kupigwa mchezo kati ya Simba ambao watawalika Azam Fc kwenye dimba la Benjamin Mkapa majira ya saa 1 usiku.
Leave a comment