TIMU ya Yanga ya jijini Dar es Salaam, imeendelea kuonesha makucha yake katika ligi kuu NBC Tanzania Bara 2021/22, kwa kujikusanyia pointi tatu muhimu. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea).
Ni baada ya kuutumia vyema Uwanja wa Majimaji, Songea mkoani Ruvuma leo Jumanne, tarehe 19 Oktoba 2021, kwa kuwafunga KMC FC ya Kinondoni 2-0.
Vijana hao wa Jangwani, walitumia dakika 11 za kipindi cha kwanza kujihakikishia ushindi.
Alikuwa ni Fiston Mayele dakika ya nne aliyeanza kupeleka shangwe kwa vijana hao wa Jangwani kwa kuunganisha pasi ya mwisho iliyochezwa na kiungo mahiri kwa sasa, Feisal Salum maarufu ‘Fei Toto.’
Yanga wakicheza kandanda safi na la kuvutia kwa kuliandama lango la vijana wa Kinondoni KMC, iliwachukua dakika saba baadaye yaani dakika ya 11, kwa Fei Toto kupiga shuti kali nje ya 18 na kwenda moja kwa moja langoni na kumwacha mlinda mlango Farouk Shikalo asijue la kufanya.
Kwa ushindi huo, Yanga imefikisha pointi tisa, baada ya kushinda mechi zote tatu alichoza. Alianza kwa ushindi wa 1-0 dhidi ya Kagera Sugar na Geit Gold Mine ambayo nayo alishinda 1-0.
Baada ya kutoka Songea kwenye mchezo huo ambao KMC wameutimia uwanja wa Majimaji kama wa nyumbani, Yanga watatua tena dimbani, tarehe 30 Oktoba 2021, kucheza na vijana wa Chamanzi, Azam FC.
Leave a comment