GOLI la dakika ya 86 lililofungwa kwa kichwa na beki kisiki wa Yanga, Lamine Moro limetosha kuwapa furaha mashabiki wa timu hiyo. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea)
Ushindi huo ilioupata leo Jumapili tarehe 13 Septemba 2020 ni wa kwanza kwa mabingwa hao wa kihistoria Tanzania kwenye Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara 2020/21.
Mchezo huo umechezwa Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam ikishudia kandanda safi kutoka kwa timu zote mbili ambazo zilikuwa zikishambulia kwa zamu.
Katika mchezo wa kwanza kwenye uwanja huo, Yanga ilitoka sare ya 1-1 na Tanzania Prisons.
Mbeya City ambayo kwenye mchezo wa kwanza ilikutaka na kipigo cha 4-0 kutoka kwa KMC FC ya Dar es Salaam, mchezo uliochezwa Uwanja wa Uhuru jijini humo.
Kwa ushindi huo, Yanga imefikisha pointi nne huku Mbeya City ikicheza mchezo wa pili Dar es Salaam ikiambulia patupu.
Baada ya kumalizika kwa mchezo, Lamine Moro aliyefunga goli pekee amesema, “Namshukuru Mungu kwa kutupa ushindi. Unaweza kuona ulikuwa mchezo wenye presha ya mpira na tunamshukuru sana Mungu kwa ushindi huu.”
Moro amesema,”tumetengeneza nafasi nyingi lakini hatukufanikiwa kuzitumia zaidi ya hii moja.”
Leave a comment