MCHEKESHAJI maarufu nchini Kenya, Eric Omondi, amekamatwa kwa kukiuka kanuni ya maadili ya Bodi ya Ukaguzi wa Filamu nchini humo (KFCB). Anaripoti Mwandishi Wetu, Kenya…(Endelea).
Taarifa kutoka ndani ya Kenya zinasema, Afisa Mkuu Mtendaji ya KFCB, Dk. Ezekiel Mutua amethibitisha kukamatwa kwake.
”Maafisa wa Ufuatiliaji wa Bodi ya Uainishaji wa Filamu Kenya, wakishirikiana na Maafisa wa Polisi kutoka Kurugenzi ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) leo Alhamisi mchana wamemkamata Eric Omondi kwa kukiuka masharti ya Sheria ya Filamu na Maonyesho ya Sura Sura 222 ya Sheria za Kenya kwa kutengeneza na kusambaza filamu ambayo haijaidhinishwa kwa jina “Wife Material,” taarifa ya Dkt. Mutua imesema.
Dk. Mutua ameweka tangazo hilo katika ukurasa wa Twitter yake kwa kutilia mkazo, kama hatua ya kutia mkazo.
Hata hivyo, taarifa kutoka nchini humo zinaeleza, hii sio mara ya kwanza Dk. Mutua na Eric Omondi kutofautiana kuhusu maudhui ya filamu hiyo.
Katika onyesho jipya la filamu hiyo, “Wife material” ya Eric Omondi inayojumuisha wahusika kutoka Kenya na Tanzania, wanaonekana wakipigana hadharani na kulazimu polisi kuingilia kati.
”Vita hivyo” vilianza wakati mmoja wa warembo hao aliangusha meza na kuvunja glasi zilizokuwa mezani na kumwaga vileo.
Video hiyo iliyosambazwa mitandaoni, imeibua mjadala kwa baadhi ya mashabiki wake wakiuliza ikiwa ni walikuwa wanaigiza au ni uhalisia.
Hatua hiyo, imemtibua Dk.Mutua, aliyetaja kuwa filamu hiyo ni “iliyooza”
Aidha Dk. Mutua amesema Bodi itachukua hatua zote zinazowezekana za kisheria kuzuia utengenezaji na maonyesho ya filamu zisizoruhusiwa kwenye jukwaa lolote linalokusudiwa kuwa maonyesho ya umma.