MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Prof. Mussa Assad, tayari yupo Dodoma “kukabiliana” na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Haki, Kinga, Maadili na Madaraka ya Bunge, kufuatia Spika wa Bunge la Jamhuri, Job Ndugai, kutoa amri ya kufika mbele ya kamati hiyo. Anaripoti Danson Kaijage, kutoka Dodoma … (endelea).
Prof. Assad anatuhumiwa na Spika Ndugai, kulidhalilisha Bunge, kufutia kauli yake kuwa mhimili huo wa kutunga sheria, ni “dhaifu.”
Hata hivyo, Prof. Asaad amekana madai hayo. Amesema, “neno dhaifu, ni neno la kawaida, tena la kiungwana kabisa, kwa wataalam wa mahesabu na limekuwa likitumika mara kadhaa katika kuripoti kazi za taasisi yangu.”
Aidha, Prof. Assad alisema kuwa alichokieleza alipokuwa nchini Marekani wakati akihojiwa na Idhaa ya Kiswadili ya Umoja wa Kimataifa (UN), ni maoni yake binafsi na akataka maoni hayo yaheshimiwe kwa mujibu wa Katiba.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa maofisa wa Bunge mjini hapa, Prof. Assad anatarajiwa kuingia ndani ya Kamati hiyo, majira ya saa nne na nusu asubuhi hii ya leo, tarehe 21 Januari.
Prof. Assad aliyeingia madarakani mwaka 2014 wakati wa utawala wa Rais Jakaya Mrisho Kikwete, alieleza katika mahojiano yake hayo na radio ya Umoja wa Mataifa (UN), kuwa kushindwa kufanyiwa kazi kwa ripoti ya ofisi yake kunatokana na “udhaifu wa bunge,” jambo ambalo linadaiwa kumkasirisha Spika Ndugai.
Alisema, “…kama tunatoa ripoti na kuna ubadhirifu na hatua hazichukuliwi, huo kwangu ni udhaifu. Bunge linatakiwa lisimamie na kuhakikisha kwamba pale kwenye matatizo hatua zinachukuliwa.”
Alikuwa akihojiwa na mwandishi wa Idhaa ya Kiswahili ya radio hiyo, Anord Kayanda, aliyetaka kujua sababu za ripoti zake kutofanyiwa kazi na Bunge.
Kamati ya Haki, Kinga, Maadili na Madaraka ya Bunge, inaongozwa na Mbunge wa Tabora Mjini (CCM), Emmanuel Adamson Mwakasaka.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka ofisi ya katibu wa Bunge, mara baada ya Prof. Assad kuripoti bungeni, atakwenda moja kwa moja kwenye ukumbi wa mahojiano uliyopo jingo la utawala na kisha kusomewa mashitaka yanayomkabili na mwanasheria wa Bunge.
Baada ya kusomewa mashitaka hayo, kanuni zinamtaka kujibu au kutojibu lolote na akiamua kujibu, ndipo wajumbe wa kamati hupata nafasi ya kumuuliza maswali.
Taarifa zinasema, baada ya Kamati kumaliza kazi yake, wanawasilisha mapendekezo ya adhabu; na au ushauri kwa Spika ambaye anaweza kuamua kuletwa bungeni ili kujadiliwa au kulimaliza jambo hilo kupitia ofisi yake.
Leave a comment