WIZARA ya Fedha na Mipango, imeliomba Bunge lipitishe bajeti ya Sh. 14.94 trilioni, kwa ajili ya matumizi yake katika mwaka wa fedha wa 2022/23, huku likitaja vipaumbele vyake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Hoja hiyo imetolewa leo Jumanne, tarehe 7 Juni 2022, bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba, akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka ujao wa fedha.
Waziri huyo wa fedha amesema, kati ya fedha hizo, Sh. 13.62 trilioni kwa ajili ya matumizi ya kawaida, wakati Sh. 1.32 trilioni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.
“Wizara ya Fedha na Mipango inawasilisha mbele ya Bunge lako tukufu, maombi ya kuidhinishiwa jumla ya Sh. 14.94 trilioni,” amesema Dk. Mwigulu.
Dk. Mwigulu amesema, Wizara ya Fedha imeomba kuidhinishiwa kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya kutekeleza vipaumbele mbalimbali, kwa kuzingatia malengo, shabaha na vipaumbele vilivyoidhinishwa katika Mpango wa Matumizi wa Muda wa Kati (MTEF) na Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa miaka mitano (2021/22-2025/26).
“Vipaumbele vya wizara ni kukusanya, kutafuta na kudhibiti mapato na matumizi ya Serikali. Kuhudumia kwa wakati deni la Serikali pindi linapoiva, kufanya tathimini ya dira ya taifa ya maendeleo 2025, kufanya tathimini ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo,” amesema DK. Mwigulu.
Dk. Mwigulu amesema “kurejesha bahati nasibu ya taifa na kufanya utafiti katika sekta za uzalishaji ili kuibua fursa za uwekezaji, uwezeshaji na vyanzo vya mapato ya Serikali katika muda mfupi, kati na mrefu. Kutekeleza maagizo ya Serikali kutafsiri Sgeria za wizara na tasisi zake kwa lugha ya Kiswahili na kuhuisha mwongozo wa taifa wa usimamizi viashiria hatarishi.”
Wakati huo huo, Dk. Mwigulu ametaja maeneo ambayo fedha hizo zitakwenda kutumika, ikiwemo, uimarishaji usimamizi mifumo ya usimamizi wa fedha za umma kupitia program ya maboresho ya usimamizi wa fedha za umma awamu ya sita, kuandaa na kujenga ghala la takwimu. Kuratibu na kusimamia zoezi la Sensa ya Watu na Makazi.
“Maeneo mengine kuziwezesha taasisi za wizara hususan taasisi za elimu na mafunzo kuboresha miundombinu ya kujifunza na kufundishia. kuendelea na ujenzi wa jengo la wizara katika mji wa Magufuli, Mtumba Dodoma,” amesema Dk. Mwigulu.
Leave a comment