WIZARA ya Elimu, Sayansi na Teknolojia nchini Tanzania imewataka maafisa elimu maalum wa halmashauri kushirikiana na maafisa elimu kata na jamii ili kuwatambua na kuhakikisha watoto wenye mahitaji maalum waliofikia umri wa kuanza shule wanaandikishwa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Hayo yamesemwa na Prof. James Mdoe, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo jana Jumanne, tarehe 18 Januari 2022 jijini Dodoma, alipokuwa akifungua kikao cha wadau wa elimu cha kupitia nyaraka za uendeshaji na viwango vya utoaji wa elimu ya awali chenye lengo la kukusanya maoni ya kuboresha nyaraka hizo zilizoandaliwa na wizara.
Profesa Mdoe alisema, Serikali imeboresha mazingira ya utoaji na upatikanaji elimu nchini ili kukidhi mahitaji ya ufundishaji na ujifunzaji na kuongeza fursa za elimu kwa makundi yote hivyo si vyema wazazi ama walezi wakawaficha watoto wenye mahitaji maalum.
“Watoto wote wana haki ya kupata elimu na ndio maana Serikali imeboresha mazingira ikiwa ni pamoja na kununua vifaa saidizi na vya kufundishia na kujifunzia ili kuondoa changamoto kwa wanafunzi, ni wajibu wa maafisa elimu kushirikisha jamii ili kuwatambua watoto waliofichwa ili wapelekwe shuleni,” amesisitiza Prof. Mdoe.
Kuhusu kikao hicho, Profesa Mdoe aliwashukuru wadau walioitikia wito wa kushiriki kikao hicho na kuwataka kutoa maoni na mapendekezo yatakayosaidia kuboresha nyaraka hizo kabla ya kutumika rasmi kwa lengo la utoaji wa elimu bora ya awali.
Kwa upande wake, Mratibu wa Malezi Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto, Hawa Suleiman alisema wizara imeandaa nyaraka mbalimbali ikiwemo Mwongozo wa Uendeshaji na Viwango katika Elimu ya Awali, Mwongozo wa Kitaifa wa Uanzishaji, Usimamizi na Uendeshaji wa Vituo Shikizi vya Shule, Kiongozi cha Uendeshaji na Viwango katika Elimu ya Awali pamoja na Zana za Upimaji wa Matokeo ya Ujifunzaji kwa michezo.
Leave a comment