WIZARA ya Afya, imetangaza nafasi za ajira 1,650 za wataalamu wa kada mbalimbali za sekta ya afya. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Nafasi hizo zimetangazwa leo Jumamosi, tarehe 16 Aprili 2022 na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Prof. Abel Makubi.
“Wizara ya Afya imepata kibali cha ajira 1,650 za watalaamu wa kada mbalimbali za afya, ambao wataajiriwa na kupangiwa vituo vya kazi ambavyo vipo chini ya uendeshaji wa moja kwa moja wa Wizara ya Afya,” imesema taarifa ya Prof. Makubi.
Kwa mujibu wa taarifa ya Prof. Makubi, katika nafasi hizo, za madaktari bingwa ni 25, madaktari (215), wafamasia (15), maafisa maabara (62), wateknolojia wa dawa, maabara, mionzi na macho (155). Mafisa uuguzi (140) na maafisa uuguzi wasaidizi (467).
Nafasi nyingi ni, wauguzi (140), wakemia (2), madaktari wa afya ya kinywa na meno (15), tabibu meno (19), watoa tiba kwa vitendo (15), wazoeza viungo kwa vitendo (31), maafisa wazoeza viungo (33), maafisa afya mazingira (40), wahandisi vifaa tiba (17), wateknolojia vita tiba (40), watunza kumbukumbu wa afya (10) na madereva (4).
Taarifa ya Prof. Makubi imesema, waombaji watakaochaguliwa watapangiwa kazi kwenye maeneo yenye upungufu mkubwa wa wataalamu wa kada za afya na hakutakuwa na kubadilisha kituo cha kazi ndani ya miaka mitatu.
Mikoa iliyotajwa kuwa ina upungufu huo na Prof. Makubi ni pamoja na, Kigoma, Katavi, Sumbawanga, Songwe, Njombe, Ruvuma, Mtwara, Lindi, Simiyu, Geita, Mara, Hospitali za Kanda za Chato na Mtwara, Hospitali ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto na vyuo vya afya.
Taarifa ya Prof. Makubi imesema, maombi hayo yatumwe ndani ya wiki mbili kuanzia leo.
Leave a comment