WIZARA ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imelaani na kukemea vikali vitendo vya ukatili dhidi ya watoto vinavyoendelea kujitokeza nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Tamko la kukemea ukatili dhidi ya watoto limetolewa leo tarehe 2 Januari 2019 na wizara ya afya ikiwa zimepita siku kadhaa tangu kutokea tukio la mwalimu wa shule ya msingi iliyoko mkoani Dodoma, kumfungia mwanafunzi ndani ya kabati.
“Vitendo hivi vinafanywa na kuhusisha ndugu na walezi wa karibu wa watoto, hivyo huzua hofu kubwa kwa watoto na jamii kwani vinaathiri malezi na makuzi ya awali ya watoto kwa kutozingatia haki zao za msingi,” inaeleza sehemu ya tamko hilo.
Aidha, Wizara ya afya imewapongeza watu walioibua tukio hilo na kuwezesha Jeshi la Polisi kumkamata mtuhumiwa wa tukio hilo kwa ajiliya uchunguzi ili sheria ichukue mkondo wake.
“Tunaamini Jeshi la Polisi watafanya upelelezi wa tukio hili kwa weledi mkubwa ili hatua stahiki za kisheria ziweze kuchukuliwa, sababu matukio ya ukatili wa watoto yanapotokea yanarudisha nyuma jitihada za serikali kulinda na kuendeleza haki na ustawi wa watoto katika ngazi ya familia ambayo ndiyo kitovu cha jamii.”
Wizara imetoa pole kwa wazazi ndugu na familia ya mtoto aliyekumbwa na mkasa huo, na kuitaka jamii kuzingatia ulinzi wa watoto ili kuwahakikishia usalama wao.
Mwanzoni mwa wiki hii mwalimu huyo anatuhumiwa kumfungia mtoto mdogo ndani ya kabati kwa kipindi kirefu na kusababisha afya ya mtoto huyo kudhoofika, pamoja na kumfanyia ukatili mama mzazi wa mtoto huyo kwa kumpiga na kumsababishia maumivu mwilini na kupelekea kulazwa.
Leave a comment