WIZARA ya Maliasili na Utalii, imejikuta katika wakati mgumu baada ya kuhojiwa kwa nini wananchi wanaoingiza mifugo katika hifadhi za wanyama pori, wanatozwa faini kubwa huku wananchi wanaoharibiwa mali zao na wanyama wanaovamia makazi, wakilipwa fidia ndogo? Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Swali hilo limeulizwa na Ester Bulaya, mbunge asiye na chama, leo tarehe 27 Aprili 2021, bungeni jijini Dodoma.
Akiuliza swali hilo, Bulaya alidai kuwa, kumekuwa na upendeleo katika viwango vinavyotozwa pindi wananchi wanapoingiza mifugo yao kwenye hifadhi hizo, na fidia zinazolipwa kwa wananchi wanaoharibiwa mali zao na wanyamapori.
“Mifugo inapoingia hifadhini, watu wanatozwa fidia, wengine fidia kubwa na hata wafugaji wamkeuwa wanapata mateso, lakini Tembo wanapoenda kwenye mazao na nyumba za wananchi fidia yake kidogo.
“Lini mtarekebisha fidia ya tembo wanapoharibu mali za wananchi ili iendane na hali halisi, kuliko hivi sasa fidia ya laki moja?” amehoji.
Akijibu swali hilo, Mary Masanja, naibu waziri wa wizara hiyo amesema, serikali iliweka viwango hivyo vya faini ili kudhibiti vitendo vya uingizaji mifugo katika hifadhi za wanayamapori.
“Ni kweli kumekuwa na changamoto hii kwamba wafugaji wanatozwa fedha kubwa kwa maana ya kiwango kilichowekwa kwenye sheria hizi, inapokuja kwa wananchi Serikai haioni umuhimu? Lakini tunachokifanya ni kukemea uingziaji mifugo katika hifadhi,”amesema Masanja.
Kuhusu wanyama kuvamia maeneo, Masanja amesema changamoto hiyo inatokana na baadhi ya wananchi kuvamia maeneo ya wanyamapori hayo.
“Nasema hivyo hawa Tembo na wanyama wengine wana serikali yao na wenyewe wanajadiliana kama tunavyojadili sisi hapa, maeneo mengi ya ushoroba wa wanyama sisi wananchi tumewafuata. Hata wao wanashangaa kwa nini maeneo yetu wanatufuata,” amesema Masanja.
Naibu waziri huyo wa Maliasili na Utalii, amewashauri wananchi walioko karibu na maeneo ya hifadhi ya wanyamapori, kupanda mazao yanayozuia wanyama hao kuvamia makazi yao, ikiwemo pilipili.
“Tembo wanaangalia nini umepanda kwenye eneo hilo, tunahamasisha wananchi waweke pilipili na kuweka mizinga ya nyuki. Kwenye hii tushirikiane, wananchi wanaaswa kutoingiza mifugo yao kwenye hifadhi,” amesema Masanja.
Leave a comment