WIZARA ya Afya nchini Tanzania imesema, ipo tayari kupokea malalamiko ya wananchi ambao hawapatiwi huduma wanazostahili. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa jana Jumatano tarehe 6 Januari 2021 na Prof. Abel Makubi, Mganga Mkuu wa Serikali baada ya kikao chake na viongozi wakuu wa sekta ya afya kwa njia ya mtandao”ZOOM.”
Kikao hicho, kiliwajumuisha waganga wakuu wa mikoa na wilaya, wajumbe wa kamati ya usismizi wa huduma za afya za mikoa (RHMT) na wilaya (CHMT) pamoja na wakurugenzi wa Hospitali za Taifa, Kanda na Maalumu.
Prof. Makubi amesema, wananchi wana matumaini na serikali yao, hivyo wanayo haki ya kusikilizwa na kutatuliwa kero zao kutoka kwa watendaji kwenye vituo vyote vya huduma za afya nchini.
Na kwamba, hivyo kamati zote zinapaswa kufanya tathimini za kero zote kwa muda wa wiki nne na kuzitatua, pia kuwasilisha ripoti Wizara ya Afya na TAMISEMI.
“Tunaanzisha utaratibu ambao sisi viongozi wa sekta ya afya tunaenda kutafuta kero kutoka kwa wananchi na kuzitatua.”
“ Hili ni agizo na tumekubaliana wasambae kwenye ngazi zote kuanzia zahanati, vituo vya afya na kwenye hospitali, tunatakiwa kuhakikisha wananchi wapate huduma bora licha ya kuwa tumeboresha huduma kwenye vituo vyetu,” amesema na kuongeza:
“Tumekubalikia suala la kuimarisha uongozi, uwajibikaji na usimamizi kwani kila mmoja ameona kuna mapungufu kwenye usimamizi wa huduma za afya nchini.
“Hivyo, tumekubaliana kila kiongozi kuanzia Taifa hadi vijijini, kusimamia sehemu zenye upungufu kwani wananchi wanahitaji mazuri kutoka kwetu, hatuwezi kuwaridhisha kwa kila kitu lakini tutapunguza matatizo yao.”
Upande wa huduma kwa wateja, amesema kitengo hicho kinatakiwa kuboreshwa kwa kuchakata kero zote za wananchi na kuzifanyia kazi.
“Viongozi hao pia wanatakiwa kukagua ndani ya hospitali zao kwenye maeneo ya kutolea dawa na stoo kuona kama dawa zipo na zinawatosheleza wananchi
“Kama kuna wizi, tuweze kuchukua hatu, waende kwenye wodi na OPD kuwasalimu wagonjwa na kama wana kero waseme ili wazitatue, pia maabara kuweza kuona kama vipimo vinafanyika,” amesema.
Kutoka Kilimanjaro Naitwa Calvin. Katika hospitali yetu ya OPD Himo kata ya Makuyuni, Kadi za kliniki kwa wajawazito hakuna. Badala yake Mama mjamzito akienda kupata huduma hiyo anaambiwa akanunue Kadi kwenye duka lililopo nje kidogo ya hospitali kwa gharama ya shilingi 2000! Hoja yangu ni kwamba: Lile kadi limeandikwa HAUZWI! Kwa maana ya kwamba hutolewa bila malipo. Sasa mbona kunakuwa na mienendo inayoudhi namna hii?😏😏