MWENYEKITI wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa, Hassan Mkopi amesema Wilaya ina mpango wa kujenga chumba kimoja cha Maabara katika kila shule ya sekondari ya kata, anaandika Christina Haule.
Mkopi amesema hayo wakati Asasi isiyo ya Kiserikali inayotoa Elimu kwa Jamii (DIRA) ilipokuwa ikitoa mafunzo katika kata 16 wilayani humo kwa ufadhili wa The Foundation For Civil Society (CFS), juu ya ufuatiliaji wa rasilimali za umma hasa sekta ya elimu ya Sekondari.
“Vifaa vyote vya maabara zote tatu tayari vimeshagawiwa kwa kila shule ya kata wilayani humo, lakini kutokana na kutokamilika kwa majengo ya vyumba havijaanza kufanya kazi” amesema Mkopi.
Amesema wilaya hiyo yenye kata 40 na vijiji 139 ina shule za sekondari za kata 26 ambazo kati yake ni shule tano pekee ndizo zilizokamilisha ujenzi wa vyumba vya maabara huku shule zingine zikiishia hatua mbalimbali za ujenzi.
Hata hivyo, amesema kutokamilika kwa majengo ya maabara katika shule hizo kumetokana na changamoto ya ongezeko la gharama za vifaa vya ujenzi ikiwemo mbao za kupaulia zilizowekwa dawa maalum ya kuua wadudu kuwa na bei kubwa.
Akizungumzia suala la kuongeza idadi ya walimu katika shule za sekondari zilizopo amesema Serikali inatambua upungufu wa walimu na kwamba itahakikisha inawaongeza.
Leave a comment