MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam kwa siku tano mfululizo, kuanzia kesho tarehe 2 Desemba 2019, itasikiliza mfululizo kesi ya uchochezi namba 112/2018 inayowakabili viongozi tisa wa Chadema, akiwemo Freeman Mbowe, mwenyekiti wa chama hicho taifa. Anaandika Faki Sosi …(endelea).
Mshtakiwa wa kwanza – Mbowe, amemaliza kujitetea Ijumaa ya tarehe 29 Novemba 2019, mshtakiwa wa pili ambaye ni Mchungaji Peter Msigwa, Mbunge wa Iringa Mjini ameenza kujitetea siku hiyo hiyo kwa kuongozwa na Wakili wa Utetezi Peter Kibatala.
Mbali na Mbowe, Msigwa, washtakiwa wengine ni Salum Mwalim, Naibu Katibu Mkuu (Chadema)-Zanzibar; John Mnyika, Naibu Katibu Mkuu – Bara; Dk. Vicent Mashinji, Katibu Mkuu wa Chadema-Taifa.
Wengine ni Ester Bulaya, Mbunge wa Bunda Mjini; Ester Matiko, Mbunge wa Tarime Mjini; John Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini; Halima Mdee, Mbunge wa Kawe.
Shauri hilo litaendelea kusikilizwa kesho tarehe 2 Desemba 2019, hadi tarehe 6 Desemba 2019, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba.
Safu ya mawakili wa serikali huongozwa na Wakili wa Serikali Mkuu, Faraja Nchimbi; Joseph Pande, Wakili wa Serikali Mwandamizi Wankyo Simon na wakili wa Serikali Salim Msemo.
Safu ya Utete huongozwa na Prof. Abdallah Safari, Kibatala wakisaidiwa na Jeremiah Mtobesya.
Viongozi hao wa chama kikuu cha upinzani nchini, wanakabiliwa na mashtaka 13 wanayodaiwa kutenda tarehe 16 Februari 2018, Kinondoni, jijini Dar es Salaam.
Wanadaiwa kufanya maandamano na kusanyiko kinyume cha sheria, yaliyosababisha uoga na hofu kwa wakazi wa Kinondoni, pia kusababisha kifo cha mwanafunzi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Akwelina Akwelin.
Leave a comment