MSEMAJI Mkuu wa Serikali, Dk. Hassan Abbasi amesema, Tanzania inaendelea na majadiliano na Benki ya Dunia (WB), kuhusu mkopo wa Dola za Marekani 500 milioni wa kuboresha sekta ya elimu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza na wanahabari jijini Dodoma, Dk. Abbasi amesema kikao cha majadiliano hayo baina ya WB na wajumbe wa serikali ya Tanzania, kinafanyika leo tarehe 30 Januari 2020.
“Stori kubwa ni majadiliano yanaendelea, serikali inazungumza na Benki ya Dunia. Walikuwa wakae siku Fulani, mmoja wa wakilishi wao akaomba waongeze siku fulani ambayo ni leo.
“Mtu unakuja leo, mshipa umekutoka mkopo umesitishwa, lazima kwenye mkopo huwezi kwenda halafu ukapewa, kuna majadiliano yanaendelea,” ameeleza Dk. Abbasi.
Dk. Abbasi amesema, serikali ina sehemu nyingi za kukopa, na inajiamini kwamba inaweza kupewa mikopo sehemu yoyote kwa kuwa ina uwezo wa kulipa.
“Sisi tunakopa mikopo mingi na kwa sababu tunaweza kulipa, unakopa haraka ili ulete maendeleo uliyopanga na una uhakika kesho na kesho kutwa utalipa.
“Kingine ni wanasiasa hao wakisema tusitumie pesa taslimu, tukikopa wanalia mnalipa sana, kesho unataka mkopo tukope mara hutaki, fanyeni tathimini kama hizo hoja kinzani zina mantiki, fuatilieni,” amesema Dk. Abbasi.
Aidha, Dk. Abbasi amewashangaa watu wanaobeza utendaji wa Serikali ya Rais John Magufuli, na kueleza kwamba viongozi wa serikali hawataki kusifiwa, pia hawataki kutukanwa na kubezwa.
“Nawaomba Watanzania kwa kutimiza wajibu wako, sisi hatutaki oya oya unamsifu Dk. Abbasi, hatutaki umsifu mtu, timiza wajibu wako, naomba kurudia leo historia inatengenezwa, usije danganya wajukuu zako ulileta maendeleo kumbe ulikuwa mpingaji mkubwa,” amesema Dk. Abbasi na kuongeza;
“Shiriki, lipa kodi, penda nchi yako na kuwa mazalendo. Kwenye changamoto eleza, usitukane, usibeze kwenye mambo usiyojua uliza utaambiwa, kuwa na mchango chanya kwenye nchi yako ili baadae ueleze kilichochema kwa wajukuu wako.”
WB ilipanga kufanya kikao cha kupiga kura za kuamua kuipa Tanzania fedha hizo za mkopo ama kutoipa, Jumanne ya tarehe 28 Januari mwaka huu, lakini kiliahirishwa baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa wanaharakati wa haki za binadamu na wanasiasa.
Wanaharakati hao na wanasiasa waliiomba WB isitoe mkopo huo kwa madai kwamba serikali haiheshimu utawala wa sheria, haki za binadamu na kukataza watoto wa kike wanaopata ujauzito shuleni, kuendelea na masomo.
Leave a comment