UMMY Mwalimu, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto amesema serikali imepokea kwa tahadhari kubwa taarifa ya uwepo mlipuko wa ugonjwa wa Ebola nchini Uganda. Anaripoti Bupe Mwakiteleko … (endelea).
Ummy amesema hayo leo tarehe 12 Juni 2019 wakati akichangia hoja kwenye taarifa ya Shirika la Afya (WHO) nchini Uganda kuhusu kuthibitishwa kwa mlipuko wa Ebola nchini humo, kupitia ukurasa wa Twitter.
Ummy ameeleza kuwa, serikali kupitia wizara ya afya imechukua hatua za utayari katika kukabiliana na ugonjwa huo.
Aidha, Ummy amewatoa hofu Watanzania huku akisema kwamba serikali itatoa taarifa zaidi kwa umma hivi karibuni kuhusu mlipuko wa ugonjwa huo.
“Tumepokea kwa Tahadhari kubwa uwepo wa ugonjwa wa #Ebola nchini Uganda.Serikali kupitia Wizara ya Afya imekuwa ikichukua hatua za utayari (preparedness) wa kukabiliana na ugonjwa huu. Wananchi wasiwe na hofu. Tutatoa Taarifa zaidi kwa umma ktk siku chache zijazo @TZMsemajiMkuu,” inaeleza taarifa ya Ummy.
Jana tarehe 11 Juni 2019 WHO nchini Uganda, ilithibitisha kwamba kuna mtoto wa miaka mitano nchini humo, ameathirika na ugonjwa wa Ebola, ambapo alikimbizwa Hospitalini baada ya kuonesha dalili za ugonjwa huo ikiwemo kutapika damu.
Taarifa zinaeleza kuwa, Taasisi ya Kupambana na Virusi nchini Uganda (UVRI) ilithibitisha kwamba mtoto huo ana ugonjwa wa Ebola.
Waziri wa Afya Uganda, Jane Ruth Aceng amesema mtoto huyo na familia yake wanachunguzwa kama wamembukizwa ugonjwa huo. Aidha, amesema watu wawili wa familia hiyo wameonesha dalili za kuwa na ugonjwa wa Ebola.
Kwa mujibu wa WHO, mtoto huyo kabla ya kuambukizwa Ebola, alivuka mpaka wa Congo nchi ambayo ni mhanga mkubwa wa mlipuko wa ugonjwa huo, siku ya Jumapaili.
Leave a comment