WAZIRI wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto Ummy Mwalimu ameishauri jamii kuwa na utaratibu na utamaduni wa kuchangiana kwenye matibabu pindi mtu anapofikwa na matatizo. Anaripoti Moses Mseti, Mwanza … (endelea).
Kauli hiyo ameitoa leo wakati akikabidhi kadi ya bima ya afya kwa watoto 105 ambazo zilizotolewa na benki ya Stanbic, jijini Mwanza.
Waziri Ummy, amesema watanzania wanpaswa kuwa na utaratibu wa kuchangiana kwenye kwenye kipindi cha misiba, tubadilike na tuanze kuchangiana katika matibabu hususani ni ya mtu kupata bima ya afya ambayo inasaidia jamii kupata huduma ya afya wakati wowote.
Ummy ametumia nafasi hiyo, kuipongeza benki ya stanbic kwa kutoa bima kwa watoto hao kwani wameonesha namna walivyo wadau katika shughuli za maendeleo pamoja na kuiunga mkono serikali ya awamu ya tano inayopambana kuhakikisha wananchi wake wanapata matibabu kwa gharama nafuu.
Aidha ameziomba taasisi na wadau wengine ambao wanashiriki katika shughuli za kijamii wahakikishe wanaelekeza katika mambo yanayowagusa wananchi ikiwemo afya ambayo mambo yote yanayofanyika ya kimaendeleo hayawezi kufanyika bila afya bora yote yatakuwa bure.
Pia amesema,ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) inaitaka Serikali kuweka mfumo wa wananchi kupata matibabu kwa urahisi,hivyo imeamua kuja na mfumo wa bima na kila mwananchi anapaswa kuwa nayo ambapo mpaka sasa wameishaanza mchakato wa sheria ambapo kabla ya septemba mwaka huu watakua wamekamilisha hatua zote.
“Bima ya afya inasaidia kupata huduma nzuri ya matibabu hivyo tutaweka utaratibu ambao ni sheria kwa kila mwananchi kuwa na bima, ambapo kwa mtoto ni shilingi 50400 kwa mwaka ambayo atapata matibabu katika hospitali zote ndani ya nchi na atahudumiwa hata kama gharama za matibabu ni kubwa.
“Tumeboresha bima ya CHF ambayo gharama yake ni 30000 kwa mwaka kwa watu sita na watahudumiwa katika vituo vya afya vya serikali na ndani ya mkoa husika, na katika kuunga mkono juhudi za stanbic nitawalipia watoto nane bima ya afya,” amesema Ummy.
Meneja wa Benki ya Stanbic tawi la Mwanza, Alphonce Mokok, amesema katika kuhakikisha uchumi unakua na maendeleo ya taifa yanaongezeka wanaamini kuwekeza katika sekta ya afya itazidi kuwa chacha ya maendeleo na kwamba wameamua kuchangia watoto hao 105 katika bima ili iwe rahisi kupata matibabu.
“Ili watoto waweze kufikia malengo na kupiga hatua katika maisha yao ni lazima wawe na afya njema, nasi tumeona bora kuwapatia bima hizo ili iwe rahisi kupata matibabu sanjari na benki kuwa karibu na jamii, ” amesema Mokok.
Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Philis Nyimbi akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mwanza, John Mongela amesema, watoto 253 kati ya 726 wanaoishi katika mazingira magumu wamepatiwa bima za afya za watoto.
Amesema watoto hao watakuwa wanapata matibabu katika vituo mbalimbali mkoani hapa, hivyo ameishukuru benki hiyo kwa kujitolea bima kwa watoto hao na kuwaomba wadau kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuchangia masuala mbalimbali ya maendekeo ikiwemo afya.
Leave a comment