WAZIRI Mkuu wa Ethiopia, Abiy Ahmed ametangaza hali ya hatari katika maeneo yote ya nchi hiyo baada ya waasi wanaopambana na wanajeshi wa Serikali kudaiwa kukaribia kuingia katika mji mkuu wa nchi hiyo Addis Ababa. Anaripoti Mwandishi Wetu… (endelea)
Hatua hiyo imekuja wakati vita hiyo ya wenyewe kwa wenyewe ikiendelea kupambana moto kwa kipindi cha zaidi ya mwaka mmoja.
Ahmed ametangaza hali ya hatari leo tarehe 3 Novemba, 2021 baada ya waasi katika jimbo la Tigray kuingia katika miji miwili muhimu kaskazini mwa nchi huku wakionekana kusonga mbele dhidi ya jeshi la shirikisho.
Inakadiriwa kuwa waasi hao wa Chama cha TPLF bado wako kilomita 400 kaskazini mwa mji mkuu wa Ethiopia na kuzidi kuiweka Serikali ya nchi hiyo katika hali ya wasiwasi.
Aidha, Waziri Mkuu huyo wa Ethiopia ametoa wito kwa raia kujilinda dhidi ya waasi.
Akiwa katika eneo la Amhara, ambako mapigano yanaripotiwa leo, ndiko alikotangaza hali ya hatari na kuajiri maelfu ya wanamgambo.
Kwa upande wa mji wa Addis Ababa, amewahimiza wakazi kuunda makundi ya kujilinda kukitokea mashambulizi ya TPLF katika mji mkuu huo.
Chama cha Tigrayan People’s Liberation Front, TPLF – kimekuwa kikipambana na jeshi la serikali kwa mwaka mzima wameungana na wapiganaji kutoka Oromo -hali inayowapa uwanja mkubwa zaidi wa kuitishia Addis Ababa.
Aidha, Waziri wa Sheria nchini humo, Gideon Timoteos amewaleza waandishi wa habari kuwa yeyote atakayetoa msaada wa kifedha, vitu au kimaadili kwa makundi ya hayo yaliyoitwa ya kigaidi, atakamatwa pia atakuwa hatarini kukabiliwa na kifungo cha miaka mitatu hadi 10 jela.
Leave a comment