WAZIRI Mkuu wa Ethiopia, Abiy Ahmed ameapishwa kutumikia muhula wa pili katika nafasi hiyo huku taifa lake likikumbwa na mzozo wa kidiplomasia juu ya vita vya Tigray. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Baada ya kuibuka mshindi katika uchaguzi huo ambao ulisusiwa na vyama vya upinzani nchini humo, Abiy ameapishwa jana tarehe 4 Oktoba, 2021 mbele ya Rais wa nchi hiyo, Sahle-Work Zewde, katika makao makuu ya Bunge la nchi hiyo.
Baada ya uapisho huo Abiy anatarajiwa kutangaza serikali yake ndani ya wiki hiyo itakayohudumu kwa kipindi cha miaka mitano.
Aidha, baada ya sherehe ndogo katika makao makuu ya Bunge, waziri mkuu mpya alielekea katika eneo la Meskel, katikati ya mji mkuu wa Ethiopia ambapo sherehe rasmi ya kutawazwa ilifanyika na Abiy kulihutubia taifa.
Kwa hafla hiyo, wakuu saba wa nchi za Afrika wamehudhuria sherehe hizo ambao ni pamoja na marais wa Uganda, Kenya, Senegal na Nigeria.
Hayo yanajiri wakati Serikali hiyo ya Ethiopia iliwafukuza maofisa saba wa UN siku moja kabla ya uapisho huo na sasa inakabiliwa na vikwazo zaidi vya Marekani.
Leave a comment