WAZIRI wa Nishati nchini Tanzania, January Makamba amesema, Serikali haijapandisha bei ya umeme huku akiagiza mamlaka kuwachukulia hatua wale wote wanaoneza uvumi huo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Makamba amesema hayo leo Ijumaa, tarehe 10 Juni 2022, wakati akijibu swali la Mbunge wa Nyasa (CCM), Mhandisi Stella Manyanya aliyetaka kujua ukweli wa taarifa zinazosambaa mitandaoni kuhusu kupanda kwa bei ya umeme.
Akijibu swali hilo, Waziri Makamba amesema, “si kweli kabisa kwamba bei ya umeme imepanda na serikali inasikitishwa na wale wanaoeneza maneno na uvumi huo na tumeomba mamlaka zichukue hatua kwa hao wanaoeneza hayo.”
Waziri huyo amesema, suala la kupandisha linaanza kwa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kupendekeza bei mpya kwa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura) kisha wananchi nao hushirikishwa.
“Kupandisha bei ni mchakato mrefu, unahusisha maombi ya Tanesco kwa Ewura na pia ni lazima wananchi wahusishwe na kushirikishwa na mchakato huo hauwezi kufanyika kwa siri.”
“Hivyo kuwa bei ya umeme imepandishwa si kweli na naomba taarifa hizo zipuuzwe na hatua zitachukuliwa kwa wahusika,” amesema
Leave a comment