KASSIM Majaliwa, Waziri Mkuu amewataka viongozi wa umma wanaojiona hawatoshi katika nafasi walizopo, waachie ngazi. Anaripoti Martin Kamote…(endelea).
Majaliwa ametoa kauli hiyo leo tarehe 26 Septemba 2019, wakati akizungumza na watumishi wa umma mkoani Iringa.
Akizungumza na watumishi hao, Majaliwa amewataka wabadilike ikiwemo kuacha kufanya kazi kwa mazoea, bali waendane na matakwa na maelekezo ya Serikali ya Awamu ya Tano.
“Muache kufanya kazi kwa mazoea, mbadilike na kuenenda sawa na matakwa na maelekezo ya Serikali ya awamu hii na anayejiona hatoshi, basi ajiondoe,” amesema Majaliwa.
Wakati huo huo, Majaliwa amewataka watumishi wa umma kutojifungia ofisini, bali wawafuate wananchi kwa ajili ya kutatua changamoto zao.
“Watalaamu tokeni ofisini nendeni kwa wananchi vijijini, mtoe elimu kwa wananchi juu ya mambo ya kitaalamu. Msiwaachie madiwani na wanasiasa kwenda kwa wananchi kutoa mambo ya kitaalamu ambayo si majukumu yao,” amehimiza Majaliwa.
Aidha, Majaliwa amewapiga marufuku Makamanda wa Jeshi la Polisi wa Wilaya (OCD)kuwapokonya wananchi mabango ya kero zao.
“Marufuku katika ziara zangu ma-OCD kuwapokonya wananchi mabango ya kero walizonazo, ukiona bango liache nilisome na kama yupo anae lalamikiwa aweze kuitwa na kujibu malalamiko hayo,”ameagiza Majaliwa.
Leave a comment