
Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
OFISI ya Waziri Mkuu imetakiwa kueleza ni lini itaacha kuwalinda wahalifu kwenye halmashauri mbalimbali nchini. Anaandika Dany Tibason … (endelea).
Kauli hiyo ilitolewa leo bungeni na Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika alipokuwa akiuliza swali la nyongeza.
Mnyika amesema kuna baadhi ya watendaji na Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Didas Masaburi wanaonyesha kiburi cha kulindwa na Ofisi ya Waziri Mkuu.
“Ni lini Ofisi ya Waziri Mkuu itaacha kuwalinda watendaji na watumishi waandamizi na kuchukua hatua…ni lini itaacha kuwalinda wahalifu?”alihoji.
Akijibu swali hilo, Naibu waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Kassim Majaliwa amesema suala la ulinzi la mtumishi mwenye makosa ndani ya mamlaka ya wizara na serikali za mitaa hilo halipo.
“Wizara haiwezi kutoa maamuzi ya moja kwa moja kama hatujapata ushaidi na kuhusisha vyombo vinavyoweza kufanya uchunguzi wa jambo hilo,”amesema .
Amesema serikali itaendelea kulifanyia kazi suala hilo ambalo linalalamikiwa hasa la Jiji la Dar es Salaam na kuchukua hatua stahiki.
Awali katika swali la msingi, Mbunge wa Viti Maalum, (CCM)Rita Kabati (CCM) alitaka kujua ni watumishi wangapi wamekamatwa na ni hatua gani walizochukuliwa kwenye upotevu wa fedha za halmashauri.
Alihoji ni kiasi gani kimepotea na kiasi gani kimerudishwa.
Akijibu swali hilo, Majaliwa amesema serikali katika kipindi cha mwaka 2010/11 mpaka 2014/15, imewachukulia hatua mbalimbali watumishi 1,205 wakiwemo wakurugenzi wa halmashauri 57 kwa kufikishwa katika vyombo vya dola, kuvuliwa madaraka, kufukuzwa kazi, kushushwa vyeo, kushushiwa mishahara na kupewa onyo.
Kuhusu fedha zilizopotea, amesema katika halmashauri ya wilaya ya Kishapu iliripotiwa upotevu wa Sh. Bilioni 6.7, halmashauri ya wilaya ya Mufindi Sh. Milioni 600 huku halmashauri ya wilaya ya Mbozi Sh. Bilioni 1.8.
Akizungumzia fedha zilizorudishwa amesema mpaka sasa jumla ya Sh. Bilioni 2.2 zimerudishwa kwenye halmashauri.
More Stories
Bei ya petroli yapaa, dizeli yashuka
Wananchi watakiwa kukipa ushirikiano kikosi kazi
NMB yatoa mikopo ya bilioni 752.7 kwa wajasiriamali wadogo na wa kati