WAZIRI wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu, Dk. Dorothy Gwajima ameipongeza Benki ya NMB kwa kutenga fedha kwa ajili ya mikopo ya wafanyabiashara wadogo maarufu kama wamachinga na kuweka huduma zitakazorahisisha utendaji kazi wa kundi hili la wafanyabiashara wadogo. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Waziri Gwajima ameyaeleza hayo alipotembelea soko la machinga la old airport la jijini Mbeya na kujionea hali halisi ya biashara za machinga katika soko hilo ambalo machinga wamehamia tangu mwaka 2020.
Waziri aliipongeza NMB kwa kutenga kiasi cha bilioni 200 kwaajili ya kuwakopesha machinga jambo ambalo litawasaidia machinga kujikwamua kiuchumi huku akiamini itakuwa chachu ya kuwatoa katika kundi la wafanyabiashara wadogo na kuingia katika wafanyabiashara wa kati na baadae wakubwa.
“Kiasi kilichotengwa na Benki ya NMB kwaajili ya kutoa mikopo kwa machinga ni kiasi kikubwa sana ambacho tunaamini machinga watatumia fursa hii kukuza biashara zao na hata baadae kukua na kuwa wafanya Biashara wa kati na wakubwa kabisa.”
“Benki hii imeamua kuwapa mikopo hii nafuu na kazi yetu machinga ni kuichangamkia fursa hii,” alisema Dk Gwajima.
“Mbali na mikopo hii ya NMB, huduma kama mikopo ya haraka kupitia simu yako ni fursa nyingine ambayo mnapaswa kuitumia ili kutatua Changamoto za upungufu wa mitaji. Kama unaweza kukopa hata laki tano kwa simu tu bila hata kufika katiwa tawi, sasa utapataje changamoto ndogondogo ya kifedha,” Dk Gwajima aliongeza.
Naye Mwenyekiti wa Shirikisho la Umoja wa Machinga Tanzania (SHIUMA), Ernest Matondo Masanja aliishukuru Benki hiyo pia kwa kuanzisha rasmi kadi za ATM maalumu kwa machinga huku akiwasihi machinga wote nchini kuunga mkono juhudi za Benki hiyo kuwainua kiuchumi.
“Mbali na kutenga fedha kwaajili ya mikopo, Benki ya NMB imetusaidia samani za zaidi ya Milioni 23 katika makao makuu yetu madogo ya jijini Dar es Salaam, lakini pia kutengeneza kadi maalumu kwaajili yetu ni jambo la kuwapongeza sana. Niwasihi machinga wote tukawaunge mkono ndugu zetu wa NMB kwani wanania ya dhati ya kutusaidia tukue kiuchumi na kuondokana na umachinga wa kudumu bali tupige hatua kimaendeleo,” alisema Ernest.
Aidha, Meneja wa Benki ya NMB kanda ya Nyanda za Juu, Straton Chilongola alitumia fursa hiyo kuwakumbusha machinga licha ya huduma bora ambazo Benki ya NMB imekuwa ikifanya kwaajili ya machinga na Watanzania kwa ujumla.
Pia kupitia benki ya NMB wanaweza kujikatia bima mbalimbali ikiwemo bima maalumu kwaajili ya machinga ambayo itawafanya wafanya shuguli zao kwa kujiamini na kutokuwa na hofu kwani itokeapo janga lolote basi Bima itafidia.
“Niendelee kuwasisitiza juu ya ukataji bima, kwani ukiwa na bima tena kwa bei ndogo sana unaweza kufidia hasara yako pindi utakapokutana na majanga ya aina yeyote.”
“Na Imani sote ni mashahidi wa ajali mbalimbali za moto ambazo zimerudish wafanyabiashara wadogo wengi nyuma sana, ila kama una bima basi hutakuwa na hofu kwani utafidia hasar yote,” alisema Straton.
Baadhi ya machinga walitoa maoni mbalimbali walipopata nafasi ya kuzungumza na waziri huku wengi wakidai juu ya uboreshaji wa miundombinu suala ambalo kaimu Mkurugenzi wa jiji la Mbeya, Triphonia Kisiga akiwahakikishia litafanyiwa kazi.
Leave a comment