WAZIRI wa Madini Dk. Doto Biteko ameitaka Bodi ya Wakurugenzi na Uongozi wa Wafanyakazi wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria watuhumiwa wa wizi wanaoliibia shirika hilo pamoja na wale wanaosambaza nyaraka za siri za shirika kwenye mitandao ya kijamii. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Waziri Biteko alimetoa kauli hiyo leo tarehe 21 Januari, 2023 wakati akifungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa shirika hilo lililoambatana na mafunzo ya magonjwa yasiyoambukiza na yanayoambukiza pamoja maadili katika utumishi wa umma.
Alisema kuna kundi la watu ndani ya shirika hilo wanafanya mambo yasiyotakiwa.
Dk. Biteko ametolea mfano kuwa Shirika hilo lilitakiwa kufutwa na Serikali 2019 lakini kipindi hicho akiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge alienda kumuomba Rais awape muda shirika hilo litaingiza faida kwa serikali.
“Rais alitukubalia ndiyo maana lipo hadi leo baada ya kutoka kuingiza faida Sh bilioni moja kwa mwaka sasa linaingiza bilioni 70 kwa mwaka.
“Kikundi cha watu hao wanaona hakuna kinachofanyika, hatutokubali hilo, wachambueni wafanyakazi hao waondoke ndani ya shirika, Nyaraka ya serikali inapigwa picha tena siyo moja faili zima na kuisambaza kwenye mtandao! haiwezekani.
“Wafanyakazi makini wanazungumzia maendeleo ya shirika siyo kutwa nzima watu na maendeleo yao, inabidi kuwaza kibiashara na siyo kusambaza majungu kwa nia huku ni kuliua,” alisema.
Alisema shirika limejaa wafanyakazi wenye shahada za juu, wanaowapa leseni wachimbaji wadogo wadogo tena walioishia darasa la saba na baada ya mwaka mmoja wanalipa kodi ya shilingi bilioni 1.
“Muda umefika sasa wa kuwa wabunifu na kuliletea tija shirika na siyo kutengeneza majungu na kusubiri mwisho wa mwezi.
“Kuna wafanyakazi wamegeuka kuwa wezi, Geita wafanyakazi wameiba lita 200,000 za mafuta ya dizeli ya kuendeshea mitambo ya kuchoronga miamba ya dhahabu. Mafuta haya yana thamani ya Sh bilioni sita, tumewakamata na vyombo vya dola vinawashugulikia na mtandao wao.
“Mnafanya wizi huo nyumbani nilikotoka hamjui kwamba vijana wa nyumbani wataniambia michongo yote mnayofanya, heri tubaki na wafanyakazi wachache kuliko kuwa na wafanyakazi wengi wezi wanaolilia kurudisha nyuma shirika, sitakubali,” alisema.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Meja Jenerali mstaafu Michael Isamuhyo alisema shirika hilo sasa limepiga hatua kubwa kimaendeleo hadi kufikia kuingiza mapato makubwa serikalini na kuaminika kwa wateja wao.
Alimweleza waziri yeye akiwa askari mstaafu atayashugulikia maagizo yote aliyowapatia.
“Haiwezekani mfanyakazi badala ya kufanya kazi zenye tija yeye anahangaika na majungu yasiyokuwa na faida katika shirika.
“Wanaofanya hivyo nafsi zao zinawasuta kwani wanajulikana wote na tutaanza kuwashugulikia mmoja baada ya mwingine hadi waishe tubaki na wafanyakazi safi wenye kujituma na kupendana na kusaidiana… shida ya mwenzako iwe yako,” alisema.
Naye Mkurugenzi wa Shirika hilo Dk. Venance Mwasse alisema shirika linapata masoko mengi ya kufanyia kazi kutokana na kuaminika na wateja wao wanaofanyia kazi.
“Mitambo ya kufanyia kazi iliyokuwa imekwama kutokana na janga la ugonjwa wa COVID- 19 imeshawasili. Tunategemea kuisimika huko Kiwira, Dodoma na Kanda ya Ziwa,” alisema.
Leave a comment